Ndugu msomaji karibu katika siku nyingine ambayo tunajifunza somo zuri sana ambalo litatusaidia kufika sehemu fulani katika maisha.
Lengo la
somo hili ni kukuonesha umuhimu wa kujifunza kuishi na watu vizuri. Kujua umuhimu
wa kuishi na watu kwa namna inavyotakiwa, itakujengea ufahamu utakaokuonesha
ulazima wa kutafuta hekima za kuishi vizuri na watu.
Zifuatazo
ni sababu za kujifunza kuishi na watu vizuri.
1.
Watu wana
vitu (vinavyoshikika) ambavyo wewe hauna.
Na kumbuka
kwenye maisha kuna vitu vingi sana unavihitaji ili ufike mbali. Na vitu hivyo
wanavyo watu, kwahiyo, ili uvipate kwa watu lazima ujifunze kuishi nao.
Hakuna mtu
atakupa kitu chake kama hauoni thamani yake, kama haujali utu wake, kama
haujali hisia zake na maeneo mengine kuhusu maisha yake. Mtu akiona utu wako
kwake, ni rahisi kutoa kitu chake ambacho kitakusaidia wewe maishani mwako.
2.
Watu wanatumiwa
na Mungu kama daraja
Ni muhimu
sana kujua kuwa Mungu anafanya kazi na watu. Kwahiyo, ukijifunza kuishi vizuri
na watu, inamrahisishia Mungu kuwatumia watu kama daraja ili wewe ufike
unapotakiwa kufika.
Kuna mahali
hauwezi kufika bila watu, hata kama unajihisi una kila kitu na unajua vingi,
utahitaji madaraja ili uvuke. Kuna watu Mungu alishawafanya kuwa daraja kwa
ajili yako, ukijua kuishi nao vizuri utafika.
Mahali fulani,
Yesu anawaambia watu kuwa alikuja kwa walio wake na walio wake hawakumpokea. Maana
yake walishindwa kuishi naye vizuri na kumbe yeye ndiye daraja la kuwafikisha
kwenye wokovu.
Kuna watu
unawachukulia poa, lakini ni daraja la Mungu kukufikisha mahali.
3.
Watu wana
ufahamu (mtazamo) unaoweza kukusaidia
Siku moja
Mkwe wake Musa alikuja, akamkuta Musa anachoka kwa sababu ya majukumu
aliyonayo, ikamlazimu kumpa ufahamu fulani wa kugawa majukumu na kuwapa watu
nafasi ili yeye abaki kwenye mambo fulani makubwa.
Mwisho wa
siku, Musa akafanyia kazi na akapata msaada kutoka kwenye changamoto ambazo
hazikuwa na ulazima. Kuna watu wana mawazo yanayoweza kukuinua na kukufanikisha
kutoka hapo ulipo.
Kuna watu
wanajua usichokijua. Ukijifunza kuishi nao vizuri, itakusaidia kupata
wanachofahamu ili ufanikiwe maishani.
Usijaribu
kuwa mjuaji, wewe haujui kila kitu, hata kama una mawazo mengi, bado kuna watu
wana mawazo ya kukusaidia kufika unapotakiwa kufika.
4.
Watu ni
rasilimali
Watu ni
rasilimali muhimu sana maishani. Kila taifa chini ya jua linathamini sana rasilimali
watu. Kila taifa linajua kuwa watu ni nguvukazi muhimu ya kusaidia kufanikisha
mambo mengi kwenye taifa.
Kuna vitu
unataka kufanya maishani. Hautaweza kufanya mwenyewe, unahitaji kufanya kazi na
watu.
Hauwezi kufanya
kila kitu peke yako maishani. Unahitaji msaada wa watu, unahitaji kufanya kazi
na watu. Unaweza kuanzisha mradi fulani au taasisi fulani ukidhani kuwa
utafanya mwenyewe lakini mbeleni utajikuta unahitaji watu.
Kadri
unavyoendelea utagundua kuwa unahitaji watu zaidi ili ufike mbali zaidi kwenye
kile unachokifanya. Kuna msemo unaosema kuwa “ukitaka kufika haraka, tembea
mwenyewe, ukitaka kufika mbali tembea na watu”. Wewe unataka kufika
mbali au unataka kufika haraka? Kumbuka harakaharaka haina baraka.
5.
Watu ni
soko
Kila bidhaa
inayozalishwa duniani soko lake ni watu. Kama hakuna watu hakuna soko. Kama haujajifunza
kujali na kuishi na watu vizuri, utashindwa kutoa kilicho bora na utashindwa
kupata wateja wa bidhaa yako.
Hata kama
una kitu kizuri kiasi gani, hata kama una bidhaa kubwa na zinazohitajika kiasi
gani, kama haujajifunza kuishi na watu na namna ya kuwahudumia watu katika
namna ifaayo lazima watakukimbia.
Unapotaka
soko lako lipanuke, walenge watu, yaani watu ndiyo kitu muhimu unachohitaji ili
kufika mbali.
Ndugu
msomaji, natumaini kupitia mambo haya matano, yamekujengea msingi unaokuonesha
ulazima wa kuishi na watu vizuri. Wakati mwingine tutajifunza kanuzi au namna
ya kuishi vizuri na watu. Mungu akubariki uwe na wakati mwema, tukutane tena
wikiendi ijayo.
Comments
Post a Comment
Thanks for your comment, God bless you!!!