MAMBO 6 YA KUZINGATIA ILI UFANIKIWE 2025

 Ndugu msomaji, hongera kuvuka mwaka 2024 na kuingia 2025. Ninamshukuru Mungu kwa ajili yako. Ametuwezesha wote kuingia mwaka huu mwingine kwa ajili ya kusudi lake maalumu.

Mungu kuturuhusu kuingia mwaka 2025 ni uhakika kuwa ametuamini, anaona tunaweza kuleta faida kwa wengine kwenye huu mwaka, anaona tunaweza kuwasaidia wengine kuwa bora zaidi ya pale walipo, tunaweza kuliishi kusudi na kufanikiwa katika mwaka huu.

Mungu ametupa mwaka, maana yake kuna neema ametoa ya kutembea katika haya majira mapya, ili kutuwezesha kufika. Hatahivyo, kuaminiwa na Mungu kunadai kuwajibika, na Mungu anahitaji kuona matokeo, na inategemea mtu aliyeaminiwa.

Kuna mambo ya kuzingatia kwa kila mtu aliyeaminiwa na Mungu ambayo yatamuwezesha kufanikiwa kwenye huu mwaka, na kumsaidia kutimiza mapenzi ya Mungu kwa majira haya.

Karibu tujifunze,

 

#1. Kaa Kwenye Uwepo wa Mungu

Hili ni jambo la kwanza kabisa la kuzingatia. Amua kukaa kwenye uwepo wa Mungu. Ni jambo lisiloepukika, huwezi kufanikiwa bila Mungu, yeye ndiye kila kitu, kama amekuamini maana yake anataka kukusaidia bila kujali madhaifu uliyonayo.

Ni, ukweli kuwa tuna maeneo mengi sana ambayo inawezekana yakawa sababu ya kutofanikiwa mwaka huu, na kwa uwezo wetu inakuwa ngumu kushughulika nayo, inamhitaji sana Mungu.

Sasa, Mungu hatafutwi wakati wa uhitaji peke yake, Mungu anatakiwa kutafutwa maisha yote, na kumtafuta Mungu ni kukaa katika uwepo wa Mungu. Amua kukaa pale. Kuna faida nyingi sana.

Uwepo wa Mungu unakupa ulinzi wa kiungu katika mali na afya yako, na tunajua kabisa kuwa hakuna mafanikio bila usalama na afya nzuri. Ukitaka kuyashinda magonjwa, hatua ya kwanza ni uwepo wa Mungu. Mimi ni ushuhuda unaoishi, nina miaka mingi siumwi, ni kwa sababu tu ya uwepo wa Mungu kwenye maisha yangu. Nakutia moyo kuwa afya yako itakuwa njema moja kwa moja unapokaa kwenye uwepo wa Mungu.

Uwepo wa Mungu unampa Mungu nafasi kwenye kukuongoza, na tunajua kuwa bila kuongozwa katika njia sahihi, tunaweza kupita katika njia yoyote na mwisho wa siku tukaishia kuangukia pua na tusifanikiwe, wengi wanaoamua kuwa wajuaji, huwa hawafiki mbali. Kwenye maisha kuna njia nyingi sana ambazo unaweza kupita, lakini Mungu anazo njia sahihi za wewe kupita. Ukikaa na yeye utapita katika njia, alizoandaa kwa ajili yako ambazo hautapotea hata kama haufahamu sana.

Uwepo wa Mungu unaleta ufunuo wa kiungu, kadri mtu anavyokaa katika uwepo wa Mungu, kuna aina ya ufahamu anaupata utokao kwa Mungu, kuna siri anaanza kuzikamata na kuishi nazo, ambazo humfanya moja kwa moja awe mbele ya wengine na mbele ya muda. Na kwenye maisha hauwezi kufanikiwa kama hauko mbele ya muda. Pia, maisha tunayoyaishi ni matokeo ya ufahamu tulionao. Unahitaji sana uwepo wa Mungu.

Uwepo wa Mungu humfanya Mungu aingilie kati katika vita zako, maisha ni vita na kila mtu anapigana ya kwake, Mungu amekuamini, haimaanishi kuwa hautakutana na vita, tena inawezekana vita zikawa kubwa kuliko 2024. Unahitaji sana msaada wa Mungu. Vita nyingi ukipigana wewe, utaishia kupoteza nguvu, fedha na rasilimali nyingine ambazo zilipaswa kutumika kukusaidia kufanikiwa kwenye mwaka. Ukikaa kwenye uwepo wa Mungu, kuna hasara unaziepuka. Kuna vita, lakini uwepo wa Mungu unampa Mungu nafasi ya kupigana kwa niaba yetu, na mwisho wa siku tunafanikiwa.

Uwepo wa Mungu unazalisha ujasiri ndani yetu, kadri tunavyozidi kukaa kwenye uwepo wa Mungu, ndivyo ambavyo ujasiri wetu unaongezeka, uimara wetu unaongezeka, hivyo tunakuwa na uwezo wa kuziendea harakati mbalimbali za maisha kwa ujasiri, na kushinda bila kujali vipingamizi vilivyopo. Ukikaa kwenye uwepo wa Mungu, kuna ujasiri wa kiungu, Mungu hajatupa roho ya woga, bali ya nguvu. Uhodari utakuwa sehemu ya maisha yako kwa kukaa kwenye uwepo wa Mungu.

Unakaa kwenye uwepo wa Mungu kwa maombi na mifungo isiyokoma; weka ratiba walau kila siku uwe na muda wa kuonekana mbele za Mungu kwa maombi, pia uwe na siku zinazoeleweka za mifungo katika wiki. Jenga tabia ya kujifunza Neno, imarisha ushirika wako na Roho Mtakatifu, azimia kuwa mtu wa ibada na uhakikishe kuwa ukienda ibadani hautoki bure. Kama haujaokoka azimia kuokoka, kama umeokoka lakini haujawa siriazi na Mungu, acha dhambi, amua kuwa siriazi, bila hivyo hautoboi. Mwaka huu azimia kukaa kwenye uwepo wa Mungu kama unataka kutoboa.

 

#2. Kuwa Mtu Wa Mipango (Malengo) Na Tathmini

Hauwezi kufanikiwa bila mipango. Usipopanga chochote utafanya chochote. Kumbuka wewe haujaruhusiwa kuja huu mwaka ili kufanya kila kitu, au kuwa mtu wa kila kitu. Kuna kitu maalumu unachopaswa kufanya na si vinginevyo. Kukosa mipango kutakufanya uwe mtu anayeishi kiholela, hautafika mahali.

Kama unaishi kiholela bila mipango, hautafika popote, hautakuwa yeyote. Kumbuka muda haujawahi kukusubiri, unapaswa kuwa na hekima ya kupangilia maisha yako, uliyopewa ndani ya mwaka mmoja yawe na maana. Weka mipango.

Watu wengi wanasema wana mipango, lakini hawaiandiki. Huku ni kujidanganya, na Mungu hawezi kufanya kazi na watu wa aina hii, tafuta watu wote kwenye maandiko, kila aliyeaminiwa na Mungu alikuwa mtu wa mipango, na Mungu mwenyewe kuna mipango aliwapa.

Hakikisha unapata muda, wa kukaa na Mungu, akusaidie kujua maeneo ambayo anahitaji wewe uwekeze kwa mwaka huu, maeneo ambayo anawaza ufanikiwe, anawaza ufanye vitu vya maana, omba msaada wa Roho Mtakatifu, kaa chini weka malengo na mikakati.

Andika malengo yako. Usijifariji kwa kuyawaza tu, yaandike, na ikiwezekana mpe mlezi wako, au baba yakow a kiroho, au mtu unayemuamini ambaye atakusaidia kukuwajibisha katika malengo yako. Acha kuweka malengo ambayo unajidanganya, weka malengo yanayofikika, acha kujiwekea malengo ambayo hautafanya chochote, na hakikisha unapoweka malengo yako, unakuwa na Roho Mtakatifu karibu, ili akusaidie maana hatuweki malengo kwa vile tulivyo nje, bali kwa vile Roho Mtakatifu anatusaidia kutokea kwenye uwezo wetu wa ndani.

Malengo yatatupa nidhamu ya muda, ukiweka malengo utagundua kuwa una muda mchache sana wa kufanya mambo yako. Ukiuona mwisho wako, na kujua kuwa una siku 366 au 365 tu, utagundua hauna tena muda wa kupoteza. Utajikuta unaacha vitu visivyo vya lazima, kama wewe ni mtu wa malengo tena yanayoandikwa, utajikuta vitu fulani unalazimika kuacha maana unagundua kuwa havikuongezei chochote kwenye kutimiza malengo yako bali vinapoteza muda wako.

Malengo yanatuonesha wapi pa kuongeza nguvu, mtu akiweka malengo, atagundua kuwa kuna maeneo mengi sana ambayo anahitaji kuyashughulikia maana ni ukweli kuwa hatafika mahali. Hii itamsaidia mtu kushughulika na udhaifu wake wote. Kuna madhaifu yanaendelea kukaa kwenye maisha yetu kwa sababu hatuna malengo na tunaishi kiholela tu. Kuna vitu hautashughulika navyo mpaka uwe na malengo. Kuna dhambi hautashughulika nazo mpaka uwe na malengo, na ukiangalia malengo hayo yanadai utakatifu.

Malengo yanatuonesha vipaumbele, kadri unavyoyaangalia malengo na kukaza kuyashika, utagundua kuna vitu vinahitaji muda wako mwingi, vingine mchache, vingine wastani na kadhalika. Ukiona una shida ya vipaumbele, ujua haujakaza katika eneo la malengo. Kumbuka kama hatufanyi vitu kwa vipaumbele hatuwezi kufanikiwa hata kidogo, kila mtu asiyejua vipaumbele, hajawahi kufika mahali, anaweza kubaki alipo na mwisho wake kupotea kabisa. Ukiwa hujui nini cha kufanya na kwa muda gani, na nini cha muhimu, nini kianze na kipi kifuate, tiba yake ni malengo. Weka malengo, utaona mambo yenye uzito zaidi.

Malengo yanaonesha nafasi ya Mungu kwetu, kila anayeweka malengo, akiyatazama kwa makini, atagundua kuwa ana mzigo mkubwa wa kubeba ambao unaamua mafanikio yake, na anaona mzigo huo anahitaji msaada kabisa, na msaada wa kwanza ni Mungu. Kadri unavyozidi kuwa mtu wa malengo, unaona namna ambavyo unamhitaji Mungu zaidi katika maisha yako. Ukiona hauoni na hauhitaji zaidi msaada wa Mungu, ni kwa sababu hauna tabia ya kuishi kwa malengo tena yaliyoandikwa.

Malengo yanatuonesha watu wa kwenda nao katika kipindi husika, unakwenda na kila mtu ni kwa sababu hauna malengo. Mara utakapoweka malengo, utaona kuna watu ni kweli unawapenda, lakini haupaswi kwenda nao, la sivyo hautafika unapotakiwa kufika kwa mwaka huu. Utagundua kuwa unahitaji aina fulani ya watu, na watu fulani uachane naye. Weka malengo, utaaanza kuona ni kina nani wa kufanya nao kazi.

Kaa chini, andika, pangilia. Weka malengo yako ya mwaka huu, usikubali kuishi kiholela.

Vilevile, unapaswa kuwa mtu wa tathmini. Ukiweka mipango, unaanza kuichukulia hatua, unapofika kila baada ya kipindi fulani hasa miezi 3, unapaswa kufanya tathmini ya namna unavyotekeleza malengo yako. Ukifanya hivi, na ukawa mwaminifu, utaona maeneo unayofanya vizuri, maeneo ambayo haufanyi vyema, na maeneo ambayo unahitaji marekebisho ili ufanikiwe. Tathmini hutupa nidhamu na ubunifu. Kila baada ya miezi mitatu, kaa chini, pitia malengo yako, angalia ulivyoyatekeleza, andika kwenye daftari lako la mwaka, andika changamoto kwa kipindi hicho, andika maazimio kwa ajili ya robo inayofauata, na uwe mtu wa tabia hiyo kila wakati. Lazima utafanikiwa.

 

#3. Jiunganishe Na Watu Sahihi

Kwenye haya maisha hauhitaji kwenda na kila mtu hata kama unampenda au kuona ni mzuri sana. Unahitaji kwenda na watu sahihi. Unahitaji kwenda na watu ambao mtafika wote salama.

Kuna watu unawahitaji ambao hao ukienda nao tu lazima ufanikiwe. Kuna watu ukienda nao lazima ufeli tu hata kama una moto kiasi gani. Hata kama una mipango mizuri kiasi gani, kama hauna watu sahihi wa kwenda nao, hautafika mahali popote.

Watu sahihi wanatupa joto njiani, kwenye mchakato wa kufanikiwa katika mwaka huu, kuna mambo mengi sana ambayo utakutana nayo, ambayo utajikuta unahisi kama uko peke yako, au unahisi baridi, watu sahihi watakuwepo kukutia moyo, na kukupa joto ambalo ni muhimu kwa ajili yako kufika safari. Ni ukweli kuwa maisha yana vipindi mbalimbali, kuna watu unawahitaji, ambao wanaenda safari kama ya kwako, ambao mtatiana moyo na kushikana mkono, itasaidia kurudi nyuma.

Watu sahihi wanatusaidia kushughulika na madhaifu yetu, kuna watu ukikaa nao, madhaifu yako yatakuwa fimbo ya kukuchapia, na usifike mahali. Lakini unapokaa na watu sahihi, wanakusaidia kushughulika na udhaifu wako, watakupa hekima na njia sahihi za kushughulika nao. Watavumilia udhaifu wako, watakusaidia na kuwa sehemu ya kuwezesha wewe kutoka kwenye hali uliyonayo. Wao wanaweza kuwa wamepita hapo, au wana hekima ya eneo hilo, ambayo itakusaidia kuvuka hapo.

Watu sahihi wanatupa mashauri sahihi, kwenye maisha haya, unahitaji mashauri sahihi katika kuyaendea mambo mbalimbali ili ufanikiwe. Usipokuwa na watu sahihi hautapata mashauri sahihi. Maandiko yanasema kwa mashauri ya akili fanya vita, na wokovu huja kwa washauri wengi (sahihi). Ukikosa hekima mbalimbali za watu, hautafika mahali. Hata Musa pamoja na kuwa na uwezo wa kuonana na Mungu, kuongea na Mungu kama mtu aongeavyo na rafiki yake, bado alihitaji mashauri ya Yethro mkwewe kuhusu ugawaji wa madaraka ambayo mwisho wa siku ikamrahisishia utekelezaji wa malengo. Wewe na mimi hatujui kila kitu, tunahitaji watu wa kutushauri katika maeneo mbalimbali.

Watu sahihi wanatuunganisha na Mungu, ukikaa na watu sahihi, watakusaidia kumuona Mungu na kuona ubora wa Mungu na namna ambavyo ni wa muhimu sana kwenye maisha yetu. Watu sahihi wanaijua nafasi ya Mungu, na wanaiheshimu na hakika watakuchagiza na kukuchochea wewe kuwa karibu na Mungu, maana hata wao wanafahamu siri ya kufanikiwa kwao, ni kuwa karibu na Mungu.

Watu sahihi wanajitoa sana kwa ajili yetu, kuna vitu ambavyo hauna uwezo wa kufanya, hali yako ya kifedha hairuhusu, ni kweli kabisa, huwa inatokea, lakini Mungu anafanya kazi na watu. Ukiwa na watu sahihi, una uhakika wa Mungu kukusaidia kupitia wao. Hawa watu huwa wanajitoa kwenye kiwango ambacho hata wewe hauwezi kurudisha walichofanya, na si hivyo tu, hautawaona wakiutumia msaada waliokupa kama fimbo ya kukuchapia na kukuendesha. Hawa watu wanajitoa sana, lakini wanaheshimu, wanathamini, na kulinda utu wako. Hata wakikusaidia, utu wako kwao ni kitu muhimu sana.

Watu sahihi ni muhimu sana lakini ni vigumu sana kuwaona, inahitaji jicho la utambuzi wa kiungu kuwaona. Hivyo, tafuta msaada wa Mungu wa kukuunganisha na hawa watu sahihi, na Mungu atawaleta kwako, na utawaona, na hao watu watakuwa baraka sana kwako. Mwaka huu azimia kuachana  na watu mbalimbali, amua kumuomba Mungu akuunganishe na watu sahihi, na muombe MUNGU awaondoe watu wasio sahihi, na akutie nguvu ya kuachana nao.

 

#4. Kuwa Mtu Wa Misingi

Ni muhimu uwe na misingi ambayo utaiishi katika mwaka huu. Uwe na mambo ambayo utayathamini sana, na utahakikisha kuwa hauyavunji. Misingi ni misimamo yako. Misingi yako ni maisha yako. Mtu akivunja misingi yako, ameyavunja maisha yako. Misingi yako ni kila kitu.

Maisha yetu yanajengwa kwenye misingi yetu, Samsoni alipoangusha nguzo (misingi) ya jengo ndivyo alivyoangusha jengo zima. Mfano, mimi mojawapo ya msingi wangu ni UWAZI. Maisha yangu yamejengwa kwenye uwazi, nikiacha kuwa muwazi, nimeharibu maisha yangu, ninaanguka. Ndiyo maana niko muwazi kila siku, na ndivyo maana nashiriki na wewe siri hizi, kwa sababu uwazi ni msingi wa maisha yangu.

Misingi inaamua tutafanya nini, msingi ndiyo mwanzo wa kila kitu na mwongozo wa ufanyaji wa kila kitu. Jinsi tunavyofanya mambo yetu ni matokeo ya misingi tuliyojiwekea ambayo tunaishi katika hiyo. Kama hauna msingi katika lolote, hautafanya chochote. Na mwisho wa siku hautakuwa chochote katika huo wakati wako wa maisha.

Misingi inaamua utambulisho wako, ukiona mtu anaonekana ni muongo, ni kwa sababu ameweka maisha yake kwenye msingi wa uongo. Uongo ni msingi wa maisha yake. Jinsi watu watakavyokuona, na kukuchukua ni matokeo ya misingi yako ya maisha. Mimi niliamua kuwa na msingi wa UTU, hivyo watu wakikutana na mimi lazima watakutana na msingi huu, watanitambua kama mtu anayethamini utu wa mtu. Nimeamua huu uwe utambulisho wangu.

Misingi inaamua mwisho wako kwenye jambo, ukiona watu hawadumu kwenye jambo wanalolifanya, ni kwa sababu hawana misingi ya maisha. Mojawapo ya vitu vinavyionifanya niwe mtu wa kudumu katika mambo yangu, ni msingi wa UAMINIFU. Nimejikuta nadumu kwenye mambo yangu, sipotei njiani, kwa sababu nalinda uaminifu wangu. Kadri ninavyolinda uaminifu, ndivyo ninavyodumu katika jambo husika. Ukiona mtu anatokea mbele za watu akawa na kipawa, kikakubalika, na baadaye akapotea ghafla, uwe na uhakika hakuwa na misingi nyuma inayomuwezesha yeye kudumu, misingi aliiyokuwa nayo, ilikuwa inamsapoti kuanguka na kupotea.

Misingi inaamua aina ya watu wakaokaa na sisi, kuna watu hata ufanye vipi hawatakaa na wewe kama misingi yako haiendani sana na kile unachosimamia, hii ni kawaida kwa maisha ya wanadamu, ndege wanaofanana huruka pamoja. Kama hauko tayari kuingalia misingi yako, na kuiishi kikamilifu, kuna watu hawatakaa na wewe hata kama una kitu kizuri. Kuna watu wana vitu vizuri, vya kuwafanikisha kabisa kwenye mwaka 2025, lakini hakuna mtu anayetaka kukaa naye kwa sababu ya misingi yake mibovu. Siyo kwamba una laana, ni kwamba misingi yako ni mibovu, na misingi ikiharibika mwenye haki atafanya nini?

Ndugu msomaji, sasa unaweza kujiuliza, je, wewe una misingi gani? Maisha yako yamejengwa katika misingi gani? Mimi ambaye ninakuletea siri hizi, maisha yangu yamejengwa katika misingi hii UTU, USAFI, UKWELI, UWAZI, UAMINIFU, MATOKEO na UFANISI. Misingi hii, ndiyo inayonifanya, niwe radhi kushiriki na wewe mambo haya, ambayo wengi hatuyajui, ninatamani na wewe ufike mahali fulani ambako watu watajifunza kupitia wewe. Mwaka huu azimia kuwa mtu wa misingi.

 

 

#5. Jilishe Chakula Sahihi

Hakikisha unakula chakula sahihi cha mwili. Usile hovyohovyo, kula chakula kwa utaratibu. Jali afya yako ya mwili, kujali afya ya mwili, siyo lazima uwe na fedha, ni maamuzi ya kujizatiti kula chakula bora katika hali hiyo hiyo uliyonayo. Pia, kujali afya, wakati mwingine ni kuacha chakula, siyo lazima ule kila siku, pata muda wa kufunga.

Pata chakula sahihi cha akili na roho. Soma vitabu, sikiliza mafundisho. Kaa na Roho Mtakatifu, hudhuria ibada ujifunze. Mimi kila mwaka ninasoma vitabu visivyopungua 50, na kusikiliza mafundisho mengi lakini ambayo ni sahihi.

Unacholisha ufahamu wako kinaamua umbali utakaoenda, Eliya alikula chakula kilichompa stamina ya kusafiri siku arobaini. Wewe unalisha nini ufahamu wako. Hauwezi kwenda mahali ambako ufahamu wako haujaenda, kadri ambavyo unasafiri kiufahamu, ndivyo ambavyo unaweza kwenda kimwili. Kadri unavyopanua ufahamu wako, ndivyo unavyojihakikisha kuwa utafika mbali. Hatufiki mbali kwa maneno, tunafika mbali kwa kiwango tunacholisha ufahamu wetu.

Unacholisha ufahamu wako kinaamua njia gani utatumia kufanikisha mambo, kadri unavyokuwa finyu kiufahamu, ndivyo unavyozidi kuwa njia finyu za kufanikisha mambo yako. Unahitaji ufahamu mpana ili kuwa na njia nyingi za kufanya mambo kwa usahihi. Mungu mwenyewe huwa anafundisha watu ili wapate faida, na hatimaye wapite katika njia iwapasayo kupita. Kuna njia ukipata lazima ufanikiwe, na hili ni zao la ufahamu wako. Kuna wakati hauoni njia, siyo kwa sababu hamna njia, ni kwa sababu ufahamu wako ni mdogo.

Unacholisha ufahamu wako kinaamua nani aje kwako, ukiwa na ufahamu dhaifu, utakuwa ni sumaku inayovuta watu dhaifu kama wewe. Kwa sababu ufahamu ulivyo ndivyo mtu alivyo. Kumbuka, hata kama unatamani kuwa na watu wa aina fulani, kama hauna ufahamu kama wa kwao, hautakaa nao meza moja. Yeyote anayetaka kufanikiwa, lazima awe na ufahamu kama wa wale waliofanikiwa katika hilo eneo.

Unacholisha ufahamu wako kinaamua mitazamo yako, mitazamo yako inajumuisha namna unavyoyaona mambo, kuyapokea na kuyaitikia. Kuna vitu unaviona ni muhimu, kwa sababau tu ya ufahamu wako, siku ufahamu wako ukibadilika, utagundua kuwa hivyo vitu siyo vya muhimu, na haupaswi kuendelea navyo. Kumbuka pia, ukiwa na ufahamu fulani, utautetea, utausambaza, kuulinda na kuuthamini. Sasa kama hauna ufahamu mzuri, utakuwa na mtazamo mbaya, ambao utaulinda, utautetea, utausambaza, na kuuthamini katika kila unalofanya. Unaweza kuona sasa maisha yako yatakuwaje.

Unacholisha ufahamu wako kinaamua Mungu atafanya kazi na wewe kwa kiwango gani, ni kweli kuwa Mungu ana nguvu nyingi sana lakini ufahamu wetu huwa kipimo cha yeye kufanya kazi na sisi. Kuna vitu akiruhusu kulingana na ufahamu wetu, hatutabaki salama. Ndiyo maana Mungu akitaka kufanya mambo kwenye maisha ya mtu, kitu muhimu cha kwanza ni kumletea ufahamu sahihi, ambao unaweka mazingira ya yeye kufanya vitu kwenye maisha yake. Ndiyo maana kabla Yesu hajazaliwa, alikuja malaika kuleta taarifa (chakula) kwa mariamu, na vilevile hata kuzaliwa kwa Yohana mbatizaji. Na mahali pengine anasema, umuite, naye ataitika, kisha atakuonesha mambo magumu, makubwa, usiyoyajua. Kwanini akuoneshe hayo? Ni kwa sababu akili yako ikiyashika, inamruhusu yeye kufanya kazi kwa kiwango hicho kwenye maisha yako.

Amua kusoma vitabu, amua kulisha ufahamu wako chakula sahihi, na chakula sahihi zaidi ni Neno la Mungu, hakikisha unaathiriwa na Neno la Mungu. Pata muda wa kujifunza, peke yako, wewe na Roho Mtakatifu na pia na wale wenye ufahamu wa kiungu. Soma Makala na mafundisho mbalimbali, msaidie na mwingine ajifunze. Mwaka huu, azimia kujifunza. Azimia kupanua ufahamu wako.

 

#6. Shughulika Na Udhaifu Wako

Hauwezi kufanikiwa bila kushughulika na udhaifu wako. Shughulika na udhaifu wako. Unahitaji kujiboresha katika maeneo hayo, ili ufike mahali kwenye maisha yako. Usiulee ubovu wako, usiizoeleee dhambi, usipuuzie ubaya unaouishi, usiufanye kuwa sehemu ya maisha yako.

Udhaifu wako ni mlango wa adui kukupoteza, shetani huwa anatafuta kuona mahali ambako una udhaifu ili akupoteze. Alienda kwa Hawa, akagundua hajayashika vizuri maelekeo waliyopewa na Mungu. Mungu amesema msile, yeye akaongeza na msiguse, na mwisho wa siku Adamu na Hawa wakaingia mkenge. Kinachokupoteza ni udhaifu wako.

Udhaifu unakuchelewesha katika hatima yako, kadri ambavyo unaulea udhaifu, ndivyo unavyopoteza muda wako na kujichelewesha. Hata kama unaonekana kuwa unafaa kuwa mtu fulani, udhaifu wako unakuchelewesha kuaminiwa kuwa mtu fulani katika eneo fulani. Hata Mungu, anataka kwanza ashughulike na udhaifu wako ndiyo akuamini.

Udhaifu unakufanya usiaminike, kadri watu wanvyozidi kujua kuwa una udhaifu fulani, ndivyo ambayo hauaminiki kwao. Mfano uwe mchungaji, halafu washirika wajue kuwa wewe ni mzinzi, uwe na uhakika kuwa kule kukuamini kwao, kutaondoka ghafla. Sauli alipoung’ang’ania udhaifu wake, Mungu hakumuamini, akatafuta mtu mwingine. Bila kujali kuwa eneo ulilopewa linafaa, kama una udhaifu, hautaaminika.

Udhaifu wako ndiyo anguko lako, watu wanaonekanaga bora kwenye vipawa vyao, lakini baada ya muda, kwa sababu ya udhaifu, hasa ule wa siri, ile dhambi ya siri, unashangaa mtu kaanguka ghafla. Kuna udhaifu alikuwa anaulea ndani yake, alipaswa kushughulika nao mapema kabla hajapewa nafasi lakini alipuuzia.

Udhaifu hukuzuia kufanya vitu, huwezi kufanya kazi ya kuwahudumia watu huku unafanya uzinzi, utasikia hukumu, utajikuta tu hauwezi kufanya huduma. Hata ukijilazimisha, huduma yako haitakuwa na matokeo. Kuna vitu hautafanya kwa sababu wewe ni dhaifu katika eneo fulani, kama wewe ni dhaifu katika matumizi ya fedha, kuna baadhi ya malengo hautayafanikisha kwa sababu unatumia fedha hovyohovyo. Kuna dhambi, inamfanya Mungu asikutumie, inakuwa kizuizi cha yeye kukupa nafasi ya kufanya makubwa.

Dhamiria kushughulika na udhaifu wako. Na udhaifu lazima ukasirike kwanini uko nao, na sehemu ya kwanza ya kuanza ni kwa Mungu, unamueleza Mungu namna ambavyo udhaifu huo unakutesa na unahitaji kutoka hapo. Kuna madhaifu mengine ni zao la vifungo fulani fulani, hivyo ukianza na Mungu itakuwa rahisi kutoka hapo.

Wakati mwingine inaweza kukulazimu kuwashirisha watu wa muhimu kama walezi, baba wa kiroho na wengine, ambao wanaaminika. Mungu huwa amewaamini na nguvu ya uponyaji katika madhaifu. Gharama ambayo wewe ungelipa miaka, yeye anatoa tamko tu au wana hekima ya kukutoa hapo. Hatahivyo, kuna madhaifu lazima tushughulike nayo wenyewe.

Baada ya kusaidiwa lazima uchuke wajibu wako, unaposhughulika na udhaifu wako, kuna mazingira utajitenga nayo, kuna watu utaachana nao, kuna vitu utaachana navyo. Kuna vitu pia utaanza kufanya. Utaanza kujenga ufahamu wako na kudumu hapo.

Udhaifu wako unaweza kuwa ni dhambi, ugonjwa, tabia, ujinga fulani na kadhalika. Shughulika nao. Mwaka huu amua kushughulika na maeneo ambayo ni dhaifu.

Ndugu msomaji, Mungu akubariki sana, ninakuombea mwaka wa mafanikio. Mungu akuongoze, na atembee pamoja na wewe, asikusahau kamwe.

 

Comments