Ndugu msomaji karibu tena katika wikiendi nyingine ambayo Mungu ametupa nafasi ya kukutana tena katika Bustani ya Ufahamu mahali ambako tunaongeza thamani zetu kila wikiendi na kuzifanya wikiendi zetu kuwa njema na kuhakikisha kuwa tunaanza wiki nyingine tukiwa na nishati mpya.
Tumekuwa katika mfululizo wa
masomo yanayohusu watu, na leo Mungu ametupa jambo jema la kujifunza tena
kuhusu watu.
Leo tutajifunza Mambo 10
Usiyoyajua Kuhusu Watu. Mambo haya yatakusaidia kujua namna unavyoweza
kuingiliana na watu katika majukumu mbalimbali na pia kufaidika na uwepo wa
watu kwenye maisha yako. Kumbuka kuwa Mungu huwa analeta watu kwenye maisha
yetu, lakini ni sisi tunaoweza kuamua kubaki na hao watu katika majira husika
na kufaidika nao.
Tunapojifunza kuhusu watu, maana
yake tunapanua mtazamo wetu kuhusu watu na utu wao ili kutusaidia kujua namna
ya kujichukua tukiwa na watu, na namna ya kuteka vilivyomo ndani yao ambavyo ni
vya faida maishani mwetu.
Twende pamoja.
Jambo La #1. Watu Ni Hazina
Kila mtu unayemuona maishani
mwako kuna kitu amebeba hata kama hukioni. Yeyote anaweza kukupa chochote, ni
wewe kujua kitu gani unaweza kupata au kuwa na ufahamu kuwa mtu yeyote anaweza
kunipa chochote.
Kila mtu ndani yake ni hazina ya
kiungu ambayo imebeba mambo mengi ya thamani ambayo ni msaada kwenye maisha
yetu.
Kila unayemuona ni hazina ambayo
inatembea. Ni bohari yenye mambo mengi ambayo inawezekana hayajulikani lakini
yapo. Hata kama anaonekana hana kitu kwa nje, anacho kitu. Ndiyo maana ukisoma Kitabu
cha Luka 19:26 inaeleza kuwa mtu asiye na kitu, ananyang’anywa hata kile
alichonacho. Uwe na uhakika kuwa hakuna mtu asiye na kitu, kila mtu ana
kitu hata kama unamuona si kitu chochote.
Ukijifunza jambo hili kuwa kila
mtu ana kitu yaani kila mtu ni hazina, itakusaidia kumheshimu kila unayemuona
bila kujali unamuona katika hali gani. Unayemuona si kitu, kama ungepewa nafasi
ya kufungua moyo wake yaani ndani yake uone yale aliyonayo, ungebaki umeduwaa
kwa sababu ndani yake kuna vitu vingi ambavyo havionekani.
Siku moja wataalamu walikaa
wakipanga kujenga lifti ili kupunguza msongamano kwenye hoteli fulani,
walipokuwa wamejadili na kujadili, akatokea mlinzi mmoja, akatoa wazo kwamba
angekuwa yeye angejenga lifti nje, wakabaki wametazamana na hiyo ikawa ndiyo
sababu ya kujengwa kwa lifti ya nje katika Hotel iitwayo El Cortez ya San Diego
na kuwa mojawapo ya sababu ya umaarufu wake.
Weka akilini kuwa, watu ni
hazina.
Jambo La #2. Watu Wanabadilika
Ni muhimu sana ufahamu kuwa watu
wanabadilika. Inawezekana haujui, ndiyo maana unapokutana na watu kuna namna
unawachukulia; unaweza kuwapuuza au kuwaona kuwa hawawezi kufanya chochote au
hawawezi kufika popote.
Mtu anaweza kubadilika na kuwa zaidi
ya vile unavyomuona. Haitoshi kusema kuwa unayemuona ndiye halisi aliyekusudiwa
kuwa, muda wowote anaweza kubadilika na kuwa yeyote katika namna usiyodhani.
Mtu yeyote anaweza kuwa yeyote
kama yatawekwa mazingira ya kumuwezesha kuwa yeyote. Watu wanabadilika,
unayemuona leo hawezi kukusaidia kesho anaweza kukusaidia katika jambo ambalo
usingeweza kudhani atakusaidia.
Sauli aliyekuwa muuaji akawa
Paulo Mtume wa yule ambaye watu wake alikuwa akiwaua na kuwatesa. Daudi mchunga
kondoo akawa mfalme, au Yusufu mtumwa kuwa mkuu wa nchi ya Misri. Watu
wanabadilika, usiwe na tabia ya kudharau watu kwa hali yao ya sasa.
Unaweza kukutana na mtu
ukampuuza, ukamfanyia mambo yasiyofaa, baada ya siku ukakutana naye mahali
ukaishia kulia na kumuomba msamaha. Mtu wa hovyo, muda wowote anaweza kuwa mtu
wa maana ambaye hajawahi kuonekana tangu kuumbwa kwa misingi ya ulimwengu.
Watu wanakua, wanapitia
michakato mbalimbali, hakuna watu wanaokaa palepale walipo, mtu anabadilika
kila wakati. Mabadiliko ni sehemu ya maisha ya mtu. Mtu hatabaki pale pale,
anaweza kwenda juu zaidi au kurudi nyuma kila baada ya mabadiliko kutokea. Watu
wanabadilika.
Jambo La #3. Ubora Wa Watu Umefungwa Katika Mazingira.
Kinachokwamisha watu kutokuwa
watu hasa, ni kutokuwepo kwa mazingira wezeshi, kwahiyo akiwa tu kwenye
mazingira yake hazuiliki, lazima awe bora kuliko vile unamuona leo.
Mfano wake ni samaki, samaki
ukimuweka nchi kavu huwezi kumuona kuwa ni bora, lakini samaki huyo huyo
ukimuweka kwenye maji, utagundua kuwa siyo kwamba hajui, ni mtaalamu katika mazingira
yake. Mfano mwingine ni tai, mazingira ya tai ni juu sana na kwenye kimbunga,
ndege mwingine haendi pale, lakini yeye huenda pale, ubora wake huonekana
kwenye kimbunga ndiyo maana hatembei na ndege wengine.
Kila mtu ana mazingira yake ya
kumfanya awe bora. Kila mtu kuna mahali akikaa, kuna nafasi akipewa, lazima
vitu bora vionekane ndani yake. Ukimlazimisha mtu kukaa katika sehemu ambayo si
yake halafu ukataka akuletee matokeo mezani ni sawa na kuulazimisha mkuyu ukupe
maembe, ni jambo lisilowezekana.
Kila mtu ana mahali pake ambako
anaweza kufanya vitu alivyoumbiwa kufanya kwa ubora kuliko vile anafanya kwa
sasa. Kadri mazingira yanavyoboreshwa ndivyo na yeye atoa kilicho bora zaidi.
Jambo La #4. Watu Wamefungwa Katika Muda
Kila mtu unayemuona amefungwa na
muda. Mambo yote yanayoonekana kwenye maisha yake, ni matokeo ya maamuzi yake
kwenye muda. Na kitu kikuu anachoweza kujutia katika makosa yake yote ni namna
alivyotumia muda wake jana.
Kila leo ya mtu ni matokeo ya
matumizi ya muda wake kwenye jana yake. Kila mtu amefungwa katika muda. Hii
inamaanisha kuwa, muda ndiyo mpaka unaoamua mtu anafanya nini kwa ubora kiasi
gani. Ukweli ni kwamba wanadamu wote wamepewa masaa 24, lakini hali za watu ni
matokeo ya maamuzi yao kwa kila saa walilokuwa nalo mkononi au sekunde
waliyoaminiwa.
Ifahamike kuwa muda ni zawadi
ambayo Mungu amewapa wanadamu ili kuwawezesha kuwa na maisha bora hapa duniani.
Hatahivyo, maisha ya mtu yanaamuliwa na mtu kwa namna anavyotumia muda wake.
Ukitaka kuiba maisha ya mtu, au kuiba mafanikio ya mtu, iba muda wake. Kadri
muda wake unavyopotea ndivyo anavyozidi kudidimia.
Vilevile, ukitaka watu
wafanikiwe katika eneo lolote, wasaidie wajue namna nzuri ya kuamua vyema
katika muda walionao. Hata wale unaowaona hawana cha maana cha kutoa, watapata
cha maana cha kutoa mara baada ya kuanza kuwa na hekima katika matumizi yao ya
muda.
Watu wengi wanazidi kudidimia
maishani kwa sababu wapo watu wanaowaibia muda kwa mitandao ya kijamii, tamthiliya
na vitu vingine vingi, ili wakati wewe unapoteza muda huko, wao wanakaa chini
na kuandaa vitu vingine, mwisho wa siku unabaki kuwa mteja wao kila siku, na
hakuna unakoenda. Kwahiyo, kama unataka kuwasaidia watu au kuwadidimiza watu,
jambo hilo limefungwa katika muda.
Ukitaka kumpa mtu msaada wa thamani
zaidi kama utapewa nafasi mara moja, msaidie kujua kutumia muda wake kwa
hekima. Hakika dunia itajivunia uwepo wake siku moja kama ataendelea kubaki
katika tabia hiyo ya kutumia vyema muda wake.
Pia, hata ukitaka kuwafanya
wanadamu wakupe fedha wewe tafuta kuwa na bidhaa ambayo inarahisisha wao
kutotoa muda mwingi kwa ajili ya kupata bidhaa hizo. Ndiyo maana kina Mama
N’tilie kila siku wanaongezekana na wanapata wateja, wanahakikisha kuwa
wanawasaidia watu ule muda ambao wangepika, wao wanapika, wanaenda kwao
kuchukua chakula, hivyo kilichotumika hapo ni muda. Watu wamenunua muda wake.
Wanaweza kupika, ila tatizo ni muda, hivyo wanahitaji kununua muda, mtu yeyote
anayelipia bidhaa analipia muda wa mtu aliokaa kununua hiyo bidhaa.
Vilevile, ukitaka watu wakupe vitu
vya thamani, au wafanye kazi na wewe kwa uhakika na uhuru na kujiamini,
hakikisha unakuwa na moyo wa kweli wa kujali muda wao
Jambo La #5. Watu Wana Nguvu
Kila mtu kuna nguvu anazo, kuna
vitu anaweza kufanya. Watu wengi wanawaona kuwa ni dhaifu tu, hawana chochote
cha kufanya, si kitu si lolote. Ni matokeo ya kutojua wanaweza kufanya vitu
gani.
Watu wengi hawawapi watu nafasi
kwa sababu wanaona madhaifu ya watu tu, hawaoni kingine. Ni kawaida ya watu
kuona madhaifu ya watu, na hiyo inawafanya washindwe kupata mazuri kutoka kwa
watu.
Ukijifunza jambo hili kwenye
maisha yako, watu watafunguka na kukupa vitu vya thamani ambavyo wengine
hawajavipata kutoka kwao. Unayemuona hana thamani, ni kwa sababu mtazamo wako
ni eneo la udhaifu tu.
Ukikaa na watu, wasaidie kujua
mambo mema wanayoweza kufanya, hata kama wao wenyewe wamejikatia tamaa maishani,
wanaona hawawezi kufanya. Unaweza kulipa gharama ya kuwatia moyo na kuwawezesha
kufanya kitu mpaka pale wanapoweza kujisimamia kabisa kikamilifu. Thawabu yako
ni kubwa kwa Mungu, lakini pia utakuwa umetoa mchango mkubwa sana wa kuzuia
watu kadhaa kuondoka na vitu vyao vya thamani, au kuzuia dunia kukosa mambo
ambayo inapaswa kuyapata kutoka kwa huyo mtu.
Kila unayemuona ni dhaifu, ana
nguvu, hata kama hauioni, akisaidiwa kujua uwezo wake, na kuwezeshwa na kutiwa
moyo wa kufanyia kazi uwezo wake, dunia itashangaa uwepo wake, maana atakuwa
mtu mwenye tija katika dunia yake.
Ndugu msomaji, ni matumaini
yangu kuwa umepata mambo mengi ya kujifunza. Ninaamini kuwa kuna hatua za
msingi unazichukua kwa kujifunza somo hili. Ni furaha yangu kuwa hautabaki nalo
peke yako, utashirikisha na wengine Bustani hii inayokuongezea thamani maishani
mwako.
Wewe ni mtu wa thamani sana hapa
duniani na mbele za Mungu, uwe na wikiendi njema yenye baraka za Mungu. Tukutane
tena wikiendi inayofuata kwa muendelezo wa somo letu.
Comments
Post a Comment
Thanks for your comment, God bless you!!!