Ndugu msomaji, karibu katika wikiendi nyingine ambayo Mungu ametupa kuwa hai tena na tupate nafasi ya kujifunza vitu vinavyoweza kuongeza thamani ya maisha yetu kama ilivyo ada.
Wikiendi
hii tunajifunza juu ya Kuongeza Thamani
Yako. Ni muhimu sana kujifunza jambo hili, ili ikusaidie kuwa mtu ambaye
unaweza kuwa na nafasi kubwa kati ya watu ili kuwasaidia watu.
Nikukumbushe
mambo kadhaa, hakuna mtu asiye na thamani. Kila unayemuona duniani ana thamani,
lakini changamoto kubwa sana ambayo inaonekana ni kuwa thamani za wengi
hazionekani. Kwahiyo, kuongeza thamani ni mchakato wa mtu kuionesha thamani
aliyonayo.
Kumbuka,
nafasi yako kati ya maisha ya watu inaamuliwa na thamani uliyonayo kati ya
watu. Kwahiyo, kila mtu amebeba ufunguo unaoamua nafasi yake kati ya watu, ukiongeza
thamani yako, umetengeneza nafasi kwenye maisha ya watu.
Ukweli
ni kuwa, hata kama watu hawakupendi, njia pekee ya kuwafanya wakupe nafasi ni
wewe kujiongezea thamani. Hata nafasi mbele za Mungu, ni matokeo ya mtu anayeiongeza
thamani yake. Kila mtu ni sawa mbele za Mungu, lakini nani anafanya kazi naye
ni matokeo ya thamani ambayo mtu ameitengeneza.
Ukitaka
watu wafanye kazi na wewe, Mungu afanye kazi na wewe, kitu bora unachoweza
kufanya ni kuhakikisha kuwa unaongeza thamani yako.
Tujifunze
zaidi kuhusu namna gani ya kuongeza thamani yako.
#1. Kanuni Ya Ufahamu
Hii ni
kanuni ya kwanza katika kuongeza thamani yako. Kanuni ya ufahamu ni kanuni
nyeti sana. Tofauti ya mtu na mtu ni ufahamu ambao kila mmoja anao. Alivyo mtu
ni matokeo ya kile anachofahamu kuhusu yeye, jamii yake na dunia yake kwa
ujumla.
Namna
pekee ya kuwa mtu anayeenda na wakati, mtu mwenye thamani kubwa zaidi, ni
kuhakikisha kuwa unajenga ufahamu wako. Ni lazima ulipe gharama ya kujifunza
zaidi mambo ya msingi ili uhakikishe kuwa unakuwa bora zaidi maishani.
Hapa
tunaangazia zaidi ni vitu gani unalisha ubongo au akili yako. Na unacholisha
akili yako hujumuisha vitu gani unaangalia, unavyosoma na kusikiliza. Wapi
unatumia muda wako zaidi. Mtandaoni huwa unajifunza nini, unasoma vitabu gani,
unaangalia muvi au aina gani ya vipindi vya televisheni.
Watu
wengi wanatamani kuwa bora maishani, lakini hawataki kulipa gharama maishani, na
matokeo yake kila siku wanabaki palepale huku wanasingizia wamerogwa. Huwezi
kufika mahali ambako akili yako haijafika.
Kwenye
maisha, utafanya unachofahamu, utaongea unachofahamu, utatetea unachofahamu, na
utalinda unachofahamu. Na mambo hayo huonesha kwa watu wengine una thamani
kiasi gani kwao.
Mwenye
ufahamu, anaweza kushirikiana na wengine na kuhakikisha wanaona thamani yake
kama ipasavyo.
#2. Kanuni Ya Maadili
Hii ni
kanuni ya pili katika kuongeza thamani yako maishani ili kutengeneza nafasi ya
kufanya kazi na Mungu na watu ukiwa hapa duniani na kuacha alama isiyofutika
unapoondoka.
Tambua
misingi yako ya maisha ya kila siku, ambayo uko tayari hata kugharimu uhai wao
kulinda hiyo misingi. Mambo ambayo utayaishi mema maishani, na hautakubali
kuyavunja bila kujali itakugharimu nini.
Ni
muhimu sana ufahamu kuwa unaweza kuwa na kipaji, lakini maadili ukakosa, na
mwisho wa siku hata thamani ya kile ulichonacho yaani kipaji, isionekane tena
kwa watu na usisikilizwe popote na yeyote na kushindwa kutimiza wito ulioitiwa
na Mungu.
Amua
kutengeneza mtindo na mfumo wa maisha ambao utaulinda na kuuishi kila siku
uwapo duniani, ambao hauendi kinyume na kanuni za Kiungu, na kuhakikisha kuwa
watu wengine wanafaidika na maisha yako hapa duniani.
Jiwekee
kanuni zitakazokuongoza, uziandike, uzifuate, na kuziishi. Angalizo, epuka
kuweka kitu ambacho hautafanya, uwe mkweli kwenye kile utaenda kufanya lakini
usiruhusu kuwa mvivu kwa kuacha kukaza kwenye maadili yako kwa sababu kadha wa
kadha.
Jenga
tabia yako, watu wengi wanapewa nafasi, lakini tabia mbaya walizonazo huwaondoa
kwenye hizo nafasi, na kumbuka thamani inaamua nafasi yako. Shika maadili yako
kama Yusufu, maana kadri unavyokaza kushika maadili unaongeza thamani yako na
thamani yako inaamua nafasi yako.
#3. Kanuni Ya Ushirika
Hii ni
kanuni ya tatu ya msingi, kanuni inayolenga ushirika wako na Mungu. Wekeza
katika uhusiano wako na Mungu. Mungu ana maeneo mengi ya kukujenga na kukufanya
uwe na thamani zaidi maishani.
Kuna
wakati unaona kuna namna haufai lakini ushirika wako na Mungu unalinda thamani
yako. Inakuhakikisha kuwa na thamani zaidi. Mungu ni wa thamani, na yeyote
anayekuja kwake, huwa na thamani, na ndiyo maana Mungu hufanya kazi na wale
ambao wanalinda ushirika wao na MUNGU.
Tenga
muda wako wa maombi, muda wa kujifunza Neno la Mungu, jiepushe na dhambi,
hudhuria ibada, wekeza muda wako katika ibada, ibada ni maisha na maisha ni
ibada.
Unamuhitaji
Mungu katika maisha yako zaidi ya unavyodhani, ni muhimu sana kuhakikisha una
ushirika naye wa ndani zaidi. Yeyote anayekaa na Mungu anabadilika kufanania
thamani itokayo kwa Mungu. Musa alivyokuwa na ushirika na Mungu, alibeba hadi
utukufu wa Mungu.
Acha
kulala lala, acha kupoteza muda, jenga ushirika wako na Mungu. Na kama unaishi
maisha ya dhambi, tubu, mrudie Mungu na Yesu Kristo mwokozi atakusaidia.
#4. Kanuni Ya Mipango Na Tathmini
Hakuna
maisha isiyo na mipango, ila tunatofautiana kile tunapanga kwenye hayo maisha.
Maisha ni matokeo ya mipango yetu, si ajali.
Ukitaka
kuongeza thamani yako, hakikisha unakuwa mtu wa malengo au mipaka. Epuka kuishi
kiholela. Hakikisha kuwa una malengo yako yam waka, ikiwezekana pia hata miaka
mitano au kumi ijayo.
Hakikisha
kuwa unaifuata hiyo mipango. Andika mipango, usiwe mtu wa maneno, anza pale
ulipo. Fanya vitu vinavyoeleweka. Kila mtu unayemuona mwenye nafasi, hufanya
kazi na watu ambao na wao ni kama yeye, mtu wa mipango, hutoa muda wake kwa mtu
wa mipango yenye tija na anayefanya kazi katika kile amepanga.
Fanya
tathmini kila baada ya miezi mitatu, angalia kama kuna haja ya kuboresha mikakati
ya kutekeleza malengo yako au mipango yako. Hakikisha unafanya tathmini ya
kweli. Hakikisha kuwa unakuwa mtu anayejua kujichukua, na anayefanya vitu
vinavyoeleweka mbele za Mungu hata kama kwa wanadamu bado havijaeleweka.
Hakikisha kuwa unaanza kufanya, siyo lazima ufanye kwa ukubwa, anza pale ulipo.
#5. Kanuni Ya Uzoefu
Hii ni
kanuni ya tano ya kuongeza thamani yako. Amua kukaa chini ya malezi ya watu
wenye uzoefu katika eneo ambalo wewe unatamani kuwa bora au unahisi Mungu
amekuita kufanya hapo.
Watu
wenye uzoefu kwenye maisha ni muhimu sana. Hakikisha una baba wa kiroho, una
walezi ambao kwao unawajibika, unatoa taarifa na maelezo ya unachofanya.
Watu
hawa ni wa muhimu sana kwa sababu itakusaidia kuwa mwajibikaji, watu wengi
wanaojaribu kujiongoza wenyewe mara nyingi huishia kuharibika na kutokuwa na
chochote cha maana cha kuwapa watu.
Hakikisha
kuwa unakuwa chini ya mtu fulani ambaye Mungu anakupa ili akulee na kukusaidia
kuwa bora. Kila mwenye nafasi, ameaminiwa mahali, ni lazima aliwekwa na mtu.
Wahenga wanasema, ukimuona kobe juu ya ukuta, ujue amewekwa, hajajiweka.
Wekeza
hapo, wewe ni wa muhimu sana, una vitu vingi sana lakini unahitajika kuwa chini
ya malezi. Wanaokulea ni kama mafundi seremala au wafinyazi, hukuboresha kadri
wanavyokuona kuna shida mahali, na kuboreshwa huku, kunakufanya ubora wako au
thamani yako kuongezeka zaidi na kuaminiwa na kumpendeza Mungu na wanadamu.
Ndugu
msomaji, naamini kwa wikiendi hii, hayo yatakusaidia sana, anza kuyafanyia
kazi, usisahau kuwa, mtu mwenye nafasi ni matokeo ya thamani yake, na thamani
ya mtu inaoneshwa kwa kuongeza vitu fulani kwenye maisha yake.
Comments
Post a Comment
Thanks for your comment, God bless you!!!