AINA TANO ZA WATU UNAOWAHITAJI MAISHANI ILI UFANIKIWE

Ndugu msomaji, karibu tena katika wikiendi nyingine, ya kuongeza thamani katika maisha yako. Na tupo katika mfululizo wa masomo yanayohusu umuhimu wa watu maishani ili ufanikiwa. Na leo tunajifunza kuhusu aina tano za watu unaowahitaji maishani ili ufanikiwe.

Katikaatika maisha kila mtu anahitaji kufanikiwa katika maeneo fulani fulani. Unaweza kutafuta kufanikiwa katika elimu, au uchumi, au mahusiano, au katika imani na kadhalika. Ni ukweli usiopingika kuwa hakuna mafanikio bila watu.

Kwahiyo, kwa sababu mafanikio yanahitaji watu, ni muhimu tujifunze ni watu gani tunaowahitaji maishani ili tufanikiwe katika eneo lolote lile.

Unahitaji aina zifuatazo za watu maishani;

 

1.    Walezi

Hii ni aina ya kwanza ya watu ambao unawahitaji maishani ili ufanikiwe. Walezi ni watu ambao wewe kibinafsi upo chini yao na wao wanakuongoza kwa namna moja au nyingine ili kukufanya kuwa bora zaidi ya ulivyo sasa katika eneo ambalo unakusudia kufanikiwa.

Anaweza kuwa mlezi wa kiroho yaani baba wa kiroho, na walezi wengine wa kawaida katika maeneo fulani fulani.

Walezi wako watakuwajibisha, watakushauri, watakufundisha, na kukuongoza, na kukuadhibu ipasapo ili kukusaidia usirudi nyuma kabisa maishani.

Hakuna mtu anayeenda mbele ambako huko mbele hakuna watu walioko huko, lazima uwe na watu ambao wamekutangulia mbele katika eneo fulani. Hao watu watakupa uzoefu muhimu wa huko unakoenda ili kukusaidia kutopoteza muda, au fedha na rasilimali nyingine ambako hakuna ulazima. Wengi kwa kukosa walezi, wamekuwa watu wa kuinuka na kuanguka na kurudi chini kabisa kwa sababu hakuna mtu wa kuwalea.

Hakikisha unakaa chini ya malezi, hakuna mtu anayetokea kama uyoga, hakuna mtu anayeaminiwa ambaye hajulikani ametoka kwenye mikono ya nani. Hakikisha unamuomba Mungu akusaidie kukupitisha katika mikono sahihi, ambapo katika mikono hiyo, hautabaki kuwa mtu wa kawaida, lazima ubadilike.

Hata kama una kitu kikubwa, bila walezi, hautakuwa mkubwa, hakikisha unakaa chini ya malezi.

 

2.    Washirika

Hii ni aina ya pili wa watu unaowahitaji maishani katika eneo lolote ili ufanikiwe. Hawa ni watu ambao mko nao pamoja. Uko nao kiwango (level) moja, na wote mnaenda mahali.

Kundi hili ni muhimu sana maishani mwako kwa sababu linakupa joto, hamasa na moto wa kuendelea mbele katika safari yako ya mafanikio. Hata Daudi alikuwa na watu 400 katika kundi hili, ambapo baadaye alikuja kufanya nao kazi akiwa mfalme.

Katika kundi hili, wapo watu ambao watafanya kazi na wewe ukiwa katika mafanikio yako. Wako watu ambao ukikaa nao unapata nguvu ya kuinuka tena, wanakusaidia kujua kuwa hauko peke yako unayepambana, hivyo usije ukajisahau na kubweteka.

Kundi hili ukikaa nalo, kazi kubwa ni kubadilishana mawazo, kushirikishana uzoefu mbalimbali katika hatua ndogondogo ambazo mnapiga, kuulizana changamoto mbalimbali ambazo zinawasaidia kuchochea hamasa ya kufatuta ufumbuzi na kusonga mbele.

Kumbuka, aina ya watu ulionao katika kundi hili, inaamua unaenda wapi. Ni kweli kuwa walezi wana nafasi zaidi, lakini kundi hili linakuwa na muda mwingi zaidi na wewe maishani kuliko kundi lolote, hivyo kama ukiwa na washirika ambao si sahihi, uwe na uhakika, bila kujali mafanikio unayopaswa kuwa nayo, hautakuwa chochote.

Kwahiyo, ni muhimu uhakikishe kuwa kwa msaada wa Mungu, katika kundi hili unakuwa na watu ambao ni sahihi, ambao kwa ushirika wenu, utajihakikishia kuwa unafika mbali.

 

3.    Wahudumiwa

Wahudumiwa ni aina ya tatu ya watu unaowahitaji maishani. Kundi hili, ni lile ambalo linakupa sababu ya kufanikiwa na kuinuka katike eneo fulani maishani.

Hapa sasa ninaangazia mafanikio yanayoacha alama maishani hata ukiondoka duniani, bado utakuwa unaishi katika maisha au mioyo ya watu.

Kile ambacho unafanya, ambacho katika hicho imekusudiwa ufanikiwe, je, watu wanafaidikaje nacho? Kwa maneno mengine, kundi hili ni watu ambao wanahudumiwa na kitu chako maishani.

Mfano wake, ni kama vile ambavyo wewe ndugu msomaji, unapata kitu kupitia mimi, wewe ni mhudumiwa, mimi ninakutumikia au ninakuhudumia kile nilichonacho. Faida yangu ni pale ninapokuhudumia, na kadri ninavyokuhudumia kwa uaminifu na kwa ubora ndivyo ninavyozidi kufanikiwa maishani katika hili eneo.

Mimi nakuwa mhudumu, wewe unakuwa mhudumiwa, ninachofanya ni huduma. Kwahiyo, ukija kwangu, unaondoka na huduma ambayo mimi nimekusudiwa kuitoa kwenye maisha yako.

Ndivyo inavyopaswa kuwa, kuna watu maishani mwako wanahitaji huduma fulani, unapaswa kuwahudumia, inaweza kuwa ni katika biashara, elimu ya mahusiano, mambo ya elimu, mambo ya imani na kadhalika. Zote zinakuwa huduma, ambazo wewe unazitoa kwenye maisha ya mtu.

Sasa, lazima ujiulize wewe umepewa kitu gani kwa ajili ya watu, ukiboreshe, na uhakikishe unakitoa kwa ufanisi na ubora kwa watu, na hapo unajitengenezea nafasi zaidi ya kufanikiwa.

 

4.     Wanafunzi

Hawa ni watu ambao wao wanajifunza katika hatua ndogondogo unazofanya. Kundi hili kazi yake ni kukuangalia, na kukufuatilia na kupata kutiwa moyo na kidogo unachofanya ili nalo lisogee mahali maishani.

Kundi hili ni muhimu sana kwako kwa sababu, linakupa chachu ya kuwa bora ziadi ya hapo ulipo. Linakufanya upige hatua zaidi ya sasa. Linakufanya ukase zaidi bila kujali magumu. Hakuna mwalimu anayekubali kushindwa kirahisi mbele ya wanafunzi wake.

Ukiishi huku ukijua kuwa pamoja na kuwa maisha ni ya kwako, lakini hayo maisha ni kwa ajili ya wengi, na kuna watu wanajifunza katika namna unaishi na kufanya unachofanya hata kama ni hatua ndogondogo, utajikuta moja kwa moja unakuwa na hekima ya kujichukua, unaongeza bidii, na unahakikisha kuwa hauwavunji moyo kwa kuharibu.

Kuna wanafunzi wako nyuma yako, hata kama wewe unajiona ni mwanafunzi, kuna wengine wanakuona ni mwalimu. Ukiishi kwa mtazamo huo, utahakikisha kuwa hauharibu maisha yako, kwa sababu kuna uwezekano wa wengi kuanguka.

Hii itakupa nidhamu ya kuishi, na hakuna mafanikio bila nidhamu, si tu kwamba unafanya kwa sababu kuna watu wanakuangalia, ila ni kwa sababu unajua Mungu amekuamini maisha yako kwa ajili ya watu wengi, hivyo hauwezi kukwepa nidhamu. Na mafanikio yanachochewa na nidhamu, kila aliyefanikiwa alikuwa na bado ana nidhamu fulani zinazotafsiri na kujenga mwendelezo wake katika eneo lolote.

 

5.     Wapinzani

Hii ni aina ya tano ya watu unaowahitaji maishani. Unahitaji kuwa na wapinzani katika safari yako. Ieleweke kuwa ninaposema wapinzani, simaanishi wewe unapingana nao, bali wao ndio wanaopingana na wewe hata kama haujui.

Kila mtu lazima awe na upinzani ili afanikiwe, lakini usitafute upinzani maishani. Kwa kila mtu anayeelekea mahali, upinzani huwa unakuja hata bila kuitwa.

Kazi ya upinzani ni kukuhakikisha kuwa, haujapendelewa kuwa hapo. Japo unaweza kuona kama wanataka kukuangusha, lakini ni wajibu wao, ili kukuthibitisha katika nafasi ambayo umeaminiwa na Mungu katika maisha yako.

Upinzani upo, ili kutusaidia kujifunza vitu ambavyo, kama tungeambiwa kwa maneno ya kawaida, tusingeweza kupokea au kuelewa. Kwahiyo, upinzani ni njia rahisi zaidi ya kutusaidia kuelewa na kukuza ufahamu wetu katika eneo husika.

Nikukumbushe, hakuna mafanikio nje ya ufahamu wako, kiwango ambacho unafanikiwa katika ufahamu, huamua kiwango cha mafanikio ya maishani.

Usizikimbie changamoto, na upinzani au wanaokuletea changamoto na upinzani, tafuta msaada wa Mungu, uwe mbunifu, ili uweze kutoka hapo na vitu vya thamani.

Kazi ya moto kwa dhahabu siyo kuiangamiza dhahabu, ni kuonesha ubora wa dhahabu ambao wengine hawauoni kwa kawaida, ndivyo ulivyo upinzani kwenye maisha yako,unafunua ubora ambao wengine hawauoni.

Ukiona kuna upinzani maishani mwako, ujue kuna kilicho bora kinatafutwa ili kitoke nje, kionekane na kiwe msaada kwa wengine, kazi yako ni kuhakikisha kuwa hicho kilicho bora kinaonekana. Usiishie na kukaa kila siku kulaumu watu wanaokupinga, jitahidi kutafuta kujua kile wanachokupinga, na kile bora kinachotafutwa, jinoe hapo, na uhakikishe kuwa unafunua huo ubora ambao wengine hawajawahi kuuona.

Upinzani wa kina Sanbalati na Tobia, ulifunua ubora wa uongozi wa Nehemia ambao haukuwa unaonekana akiwa mnyweshaji wa mfalme. Na kumfanya kuaminiwa kuwa liwali ya Yuda.

Ndugu msomaji, ni imani yangu kuwa, unazidi kujijenga kiufahamu katika eneo hili, una unazidi kujiongezea thamani, ninakuombea uwe na wikiendi njema, na uendelee kufaidi thamani zilizoko humu. ukiweza kumshirikisha na mwingine, utakuwa umesaidia kuwaongezea wengine thamani, hakikisha una marafiki wanaojua chimbo ambalo linakuongezea thamani kila siku.

Mungu akubariki!!

Comments