MAMBO 10 USIYOYAJUA KUHUSU WATU - Sehemu ya 2

 Ndugu msomaji, karibu katika wikiendi nyingine ambayo tunaendelea na somo letu kuhusu, Mambo 10 Usiyoajua Kuhusu Watu.

Katika wiki iliyopita, tuliishia katika jambo la tao, karibu tuendelee na jambo la sita na kuzidi kuongeza thamani ya maisha yetu.


        Jambo La #6. Watu Wana Udhaifu

Bila kujali mtu ni mkuu kiasi gani katika ulimwengu, bado kuna udhaifu anao. Udhaifu huo ni muhimu kwa sababu unamsaidia kuona haja ya kuhitaji msaada kwenye maisha yake kutoka kwa Mungu na wengine.

Hata Paulo alikuwa na udhaifu ambao ulimfanya awe mnyenyekevu na kuhitaji msaada wa Mungu kila wakati. Ukijua kuwa watu wana madhaifu, hautajiona kuwa wewe peke yako ni sahihi na pia wanapoharibu utajifunza kuwasaidia na kuwarejeza katika upendo bila kuathiri kanuni zilizowekwa zinazoendesha maisha ya watu hapa duniani.

Kila mtu kuna mahali ana udhaifu fulania ambao anahitaji msaada. Hata mimi kuna udhaifu ambao unanifanya niwe mwanadamu kamili, na udhaifu huu zaidi sana unanifanya kuwa karibu na Mungu, kwa sababu bila msaada wa Mungu siwezi kushinda udhaifu ambao wakati mwingine unaweza kuleta mateso maishani.

Udhaifu wa mtu haupaswi kumfanya mtu aubebe na kushindwa kuchukua hatua sahihi za kumsaidia. Udhaifu wowote unaomshinda mwanadamu, unahitaji msaada wa Mungu wa Mbinguni. Kwahiyo, kama kuna mtu unamuona ana udhaifu, au wewe una udhaifu, kitu muhimu zaidi unachoweza kufanya ni kumrudia Mungu na kumpa nafasi ya kukusaidia katika huo udhaifu.

Hakuna mjanja zaidi ya mwingine maishani. Kila mtu anapambana vita yake dhidi ya udhaifu fulani, lakini wale wanaoonekana kushinda ni matokeo ya msaada wa Mungu maishani mwao.

Ukijua kuwa watu wana udhaifu, hautashangaa kumuona mtu akija kwako kukueleza namna anavyotesekea, na hautatumia nafasi hiyo ili kuyaharibu maisha yake, badala yake utamsaidia kumuonesha njia sahihi na bora ya kuvuka hapo anapoteseka.

Kuna madhaifu ambayo yanaondoka, na kuna madhaifu ambayo yapo tu. Na hayo yote yapo kwa watu unaokutana nao kila siku, unaoshirikiana nao kila siku pale kazini. Wanahitaji msaada, wanahitaji kutegemeana ili wazidi kuwa bora kuliko hapo walipo kwa sasa. Usimdharau wala kumcheka mtu, au kumpuuzia kwa sababu ya udhaifu wake, siku moja ataota nywele zake na atawaangusha wafilisti. Udhaifu wa mtu, ni sehemu ya Mungu kudhihirisha nguvu zake kwa wanadamu.

 

Jambo La #7. Watu Wanahitaji Watu

Hili ni jambo lingine, ambalo unapaswa kulifahamu kwa undani sana kwenye maisha yako. Kila mtu kuna mtu anamhitaji maishani mwake. Huyu anahitaji mume, yule anahitaji mtoto, yule anahitaji mke, na yule anahitaji mfanyakazi, huku mwingine anahitaji mwalimu, mwingine anahitaji kiongozi na kadhalika.

Maisha ni mfumo wa utegemezi wa watu na watu. Tunategemeana watu wote. Kila mtu ana sehemu yake duniani. Hakuna mtu ambaye dunia ni yake peke yake, dunia ni yetu sote.

Kuna watu wanajihisi wao ndiyo wanaopaswa kuwepo duniani, wengine waondoke tu, hawana faida. Hatuwezi kuzuia mfumo aliouweka Mungu usifanye kazi, kila mtu anamhitaji mwingine. Unahitaji watu ili ufanikiwe.

Kama wewe ni mfanyabiashara basi utahitaji wateja. Hakuna mwalimu bila wanafunzi, hakuna mchungaji bila washirika, hakuna kiongozi bila washirika. Hakuna mtu bila watu. Tunahitajiana kuliko kawaida.

Dunia yetu, au jamii yetu, au nchi yetu iwe salama, inahitaji watu waje pamoja. Watu wanahitajiana katika maeneo mbalimbali. Hatahivyo, watu ili waje pamoja na watu, inahitaji kanuni mbalimbali za kuwaweka pamoja la sivyo uharibifu hautaepukika. Popote walipo watu kuna hatari ya uharibifu kama hakuna kanuni zinazoongoza ushirika wao.

Ni muhimu ujue kuwa unahitaji watu kwenye maisha yako ili ufike mahali. Usidharau watu, usijione umefika, hakuna mtu aliye peke yake akafika popote. Hata Adamu alihitaji uwepo wa Hawa. Tena ni Mungu mwenyewe aliona kuwa Adamu hapaswi kuwa peke yake. Mungu ameshaona kuwa haupaswi kuwa peke yako, kaa na watu. Kila mtu ana kitu cha thamani. Ishi na watu vizuri.

Kilichokushinda wewe kuna watu wanakiweza, usichofanya wewe kuna watu wanafanya, usichojua wewe kuna watu wanajua. Unahitaji watu maishani mwako kuliko unavyodhani. Lakini inamhitaji Mungu zaidi ili kupata watu sahihi maishani mwako.

 

Jambo La #8. Watu Wamefungwa Na Ibada

Kila mtu anaabudu. Iwe ni Mungu wa Kweli au mungu mwingine wa uongo. Kila mtu kuna anachoabudu, hakuna mtu ambaye anakwambia haabudu. Swali gumu la kujiuliza ni hili, je, anaachoabudu au anayemuabudu ndiye anayepaswa kuabudiwa?

Kila mwanadamu anahitaji ibada. Ndiyo maana popote linapotokea janga fulani lazima watu waambiane kuwa tutakuwa tumemkosea Mungu, tukatubu, Mungu atatusaidia.

Kila mtu anamhitaji Mungu. Mojawapo ya mambo ambayo unaweza kumsaidia mwanadamu, ni kumsaidia kumshirikisha juu ya ibada na Mungu wa kweli anayepaswa kuabudiwa na watu wote kwa ajili ya faida ya maisha yake.

Huwezi kujitenga na ibada, ila unaweza kuamua unaabudu nini? Kuna anayeabudu Mungu wa kweli, kuna anayeabudu milima na miti au mizimu, au fedha na vingine vingi, ni ibada. Lakini ifahamike kuwa kuna Mungu mmoja anayepaswa kuabudiwa, na siyo kila anayeabudiwa ni sahihi kuabudiwa hata kama anaabudiwa na watu wengi au wachache na kusifiwa kuwa anafanya kazi.

Muhimu sana kuwa na uhakika na unakoabudu kuwa je, ni mahali sahihi? Ushauri wangu kwako ni huu, kama unaona kuna namna ibada yako haikusaidii, basi kuna mahali pana shida, tafuta namna mrudie Mungu wa kweli akusaidie.

Ndugu msomaji, fanya toba ya kweli, kama haumwabudu Mungu wa Kweli, mrudie Mungu. Au kama kuna mtu unamuona hafanyi ibada ya kweli, msaidie amrudie Mungu wa kweli, maana ili ibada iwe ya kweli na sahihi, lazima mtu amuabudu Mungu wa kweli katika ibada yake. Mungu wa kweli, anapatikana kupitia njia moja, nayo ni njia ya Yesu Kristo. Watu wana njia (dini) nyingi za kumtafuta Mungu wa Kweli, lakini njia sahihi zaidi ni kupitia Yesu Kristo. Ukiweza kuijua njia hiyo, utagundua mengi ambayo huyajui kuhusu maisha yako na Mungu katika ibada yako.

 

Jambo La #9. Watu Wana Maswali

Kila mtu kuna swali analotafuta jibu lake. Ndiyo maana tasnia ya habari inazidi kushika kasi ulimwenguni, ulimwengu tulionao unaitwa ulimwengu au zama za taarifa. Hii ni kwa sababu, taarifa hizo zinalenga kujibu maswali ya watu ya kila siku.

Ukitafuta kujua maswali ya watu, na kuja na majibu sahihi, hakika utafaidika na uwepo wa watu duniani. Kila mtu mwenye soko duniani, ni matokeo ya kuuza taarifa au kitu fulani ambacho kinajibu maswali ya watu duniani.

Kuna watu wana maswali katika ndoa, malezi, uchumi, fedha, uongozi, elimu na kadhalika, wanahitaji majibu. Kila siku maswali yanajitokeza na yanahitaji majibu.

Watu wana shida mbalimbali wanhitaji msaada, watu wana changamoto wanazopitia, watu wana mambo yanayowayumbisha na kuwaumiza vichwa, wanatafuta kujua wanatokaje hapo. Akitokea mtu mwenye majibu, lazima apate soko, lazima apate nafasi kwenye maisha yao.

Unaweza usijue wanajiuliza maswali gani na majibu gani sahihi, lakini ukipata muda wa kutulia mbele za Mungu, na kushiriki mambo mbalimbali ya wanadamu, utasemeshwa mambo ambayo Mungu anatarajia kuona yakiwa majibu kwenye maisha ya watu na maswali ambayo watu wanajiuliza na bado hawajapata msaada.

Hii dunia haitakuja iishe maswali mpaka mwisho wake. Lazima uweke hili kichwani. Hivyo, kitu pekee unachoweza kufanya, ni kujua maswali gani yanaulizwa, na Mungu anakupa kujibu swali gani. Ukipata majibu ya hata swali moja tu, lazima usikilizwe na watu, lazima utapewa kipaumbele.

Mwenye majibu, hata awe na mwonekano usiowapendeza watu, au asipendwe na watu, bado atakuwa na nafasi kati ya watu. Kinachompa nafasi ni majibu aliyobeba. Siyo lazima ujipendekeze kwa watu ili upate nafasi ya kusikilizwa, jipendekeze kwa Mungu, akupe majibu ya maswali fulani, uje nayo, uone kama hautasikilizwa. Itafika mahali unatamani kupumzika lakini hamna muda, watu wanakutafuta kama lulu, wanatafuta majibu yao, wanaamini unayo wewe, inawezekana ni Mungu anayewaelekeza waje kwako.

 

Jambo La #10. Watu Wapo Safarini

Maisha ni gari iliyowabeba watu kuelekea mahali fulani. Watu wapo safarini. Hapa duniani kila mtu ana safari yake, kuna mtu anaelekea pale juu serikalini, kuna mtu anaelekea pale kwenye zile fedha, mwingine anaelekea kule kwenye umasikini. Na suala la mwisho wa safari yako ni wapi, ni matokeo ya maamuzi ya mtu akiwa ndani ya gari la maisha.

Vilevile, watu wapo safarini, hawaishii hapa tu duniani. Kila mtu kuna mahali anaenda, kuna wanaojiandaa kwenda Jehanamu, kuna wanaojiandaa kwenda Paradiso, kila mtu kuna mahali anaenda.

Ndugu msomaji, hakuna mtu ambaye ataishia hapa duniani. Hili ni jambo unalopaswa kufahamu, hata wewe upo safarini, na utaishia wapi ni matokeo ya umepanda gari gani hapa. Kuna gari (maisha) inayowapeleka watu pabaya, na wengine wapo kwenye gari (maisha) inayowapeleka watu uzimani.

Umewahi kuwaza utakuwa wapi baada ya kuondoka hapa duniani? Asikudanganye mtu kuwa ukiondoka duniani, kila kitu kimeisha, bado kuna mengi yanaendelea huko unakoenda, ambayo hata ya duniani huku hayafiki hata nusu. Huko ni milele, hakuna miaka 100 au 60, ni milele.

Hebu waza, mtu kwa maisha ya hapa tu duniani ambayo anaishi miaka 100 au 60 lakini analalamika kila siku kwa magumu yake, sasa itakuwaje siku atakapoingia kule jehanamu ambako ataishi milele kwa maisha mabovu anayoishi leo?

Umewahi kuwaza namna ambavyo watu wanajidanganya kwa kujifariji kuwa watasamehewa kwa maombi ya watu fulani fulani hapa duniani? Umewahi kuwaza namna ambavyo watu wanawazaga juu ya yale maombi ya Mungu mlaze mahali pema peponi? Hakuna hata mojawapo linalofanyiwa kazi, kila mtu atakula matunda ya maamuzi yake kwenye miaka michache aliyopewa duniani. Kitu muhimu mtu anachoweza kufanya ni kuamua sasa ataishi wapi baada ya maisha ya hapa duniani.

Kila mtu yupo safarini, kuna mahali anaenda. Hakuna ambaye ataishia duniani. Hilo likae ndani kabisa ya moyo wako. Kinachozikwaga pale kaburini ni mwili, na ndiyo maana unaitwa mwili wa marehemu, na siyo marehemu mwenyewe, marehemu mwenyewe hayupo, ameenda kula matunda ya kazi na maisha yake hapa duniani.

Kama unajua jambo hili, hekima bora unayoweza kuifanya ni kutubu, kubadili njia zako na kumrudia Mungu. Na hakuna njia nyingine ya kumrudia Mungu isipokuwa kwa YESU KRISTO. Ni ukweli kuwa ukiwa hapa duniani, kuna mambo mengi yanayokuzuia kuwa mtu wa haki na mtakatifu, na hapo ndipo penye ulazima wa kumkubali Yesu Kristo akupe siri zinazowafanya watu kuishi maisha matakatifu wakiwa hapa duniani. Mtu anayejifariji kuwa hakuna mtu anayeweza kuishi maisha matakatifu hapa duniani, ni kwa sababu hajaamua kumpa Yesu maisha yake ili amsaidie, yeyote aliyempa nafasi kweli kweli, maisha matakatifu yanawezekana.

Comments