Ndugu msomaji, karibu katika wikiendi nyingine, ambayo tunajifunza mambo ya kutuongezea thamani na kuyafanya maisha yetu kuwa na matokeo katika dunia yetu na tuishi maisha ya alama isiyofutika.
Wikiendi
hii, tunajifunza kuhusiana na sababu 5 za Mungu kufanya kazi na watu. Zipo
sababu nyingi, lakini leo tutajifunza sababu 5 ambazo katika hizo,
zitatuongezea thamani na kuzaa mabadiliko.
Karibu
tujifunze,
1.
Watu Wametoka
Kwa Mungu
Kila mtu
unayemuona duniani ametoka kwa Mungu. Hata awe mbaya kiasi gani, ubaya wake ni
matokeo ya hali fulani alizokutana nazo hapa duniani, na asili ya dhambi kwenye
maisha ya mwanadamu, lakini yeye mwenyewe ni matokeo ya wazo la Mungu.
Kila
mwanadamu unayemuona ni wazo la Mungu. Ametoka kwa Mungu, na kama ametoka kwa
Mungu kuna sababu iliyomfanya Mungu amlete huyu mtu ambaye tunamuona katika
mwili.
Kwa
maneno mengine, tunayemuona katika mwili, si mwili, ni mtu kutoka kwa Mungu
ambaye amebeba ajenda fulani ndani yake ya kutekeleza katika dunia ambayo
wanadamu wengine wanaishi.
Mungu
hajawahi kufanya kazi ya bahati mbaya, kila mwanadamu anayemleta amekuja kwa
kusudi. Ni muhimu kujua kuwa wanadamu wametoka kwa Mungu, na kama wametoka kwa
Mungu kuna kitu wanacho, wametumwa kufanya kazi fulani.
Mwanadamu
ni kiumbe wa rohoni aliyevaa mwili, na kiumbe huyu ametoka kwa Mungu, na
amekuja duniani kwa sababu maalumu, yupo kikazi. Ndiyo maana Mungu anafanya
naye kazi.
Mungu
anaweza kumtumia yeyote, kwa sababu wote wametoka kwake. Hakuna ambaye
alijileta mwenyewe, au aliletwa na shetani, kila mwanadamu, ameletwa na Mungu,
uwepo wake ni ruhusa kamili ya Mungu Muumbaji wa vyote.
Mungu
analazimika kufanya kazi na mwanadamu kwa sababu yeye ndiye amemleta, na kuna
vitu amempa ambavyo vinapaswa kuwafikia wanadamu. Yeye ametoka kwake, na
amekuja duniani kwa sababu yake (Mungu) na anafanya kazi kwa niaba yake (Mungu)
na ndiyo maana lazima afanye naye kazi. Kumbuka kuwa hakuna kinachotoka kwa
Mungu kisicho na kazi, kila kinachotoka kwa Mungu kina kazi yake, lazima
kitumiwe na Mungu. Kama MBINGU NA NCHI ZINAHUBIRI UTUKUFU WAKE, SEMBUSE
MWANADAMU?
2.
Watu Wana
Asili Ya Mungu (wana baadhi ya tabia za Mungu na wanaweza kuwa na tabia ambazo
Mungu anawaruhusu kuwa nazo)
Kila
mwanadamu unayemuona ana asili ya Mungu. Kuna tabia za Mungu zimefungwa ndani
yake. Mojawapo ya asili ya Mungu ni utashi au kwa lugha nyepesi uwezo wa
kufikiri na kufanya maamuzi.
Kila
mwanadamu anaweza kufanya maamuzi. Kila mwanadamu anaweza kufikiri. Hata kama
anafanya maamuzi mabaya, au kufiriki vibaya, bado yeye anaweza kutumiwa na
Mungu, na kama atatengenezewa mazingira mazuri ya kurekebisha uwezo wake wa
kufikiri na kuamua, atafanya kazi na Mungu wakati wote.
Mungu amempa
mwanadamu baadhi ya tabia zake ili kumuwezesha mwanadamu kufanya naye kazi au
kumtumia kwa ajili ya majukumu mbalimbali. Mwanadamu kuwa na asili ya Mungu,
kunampa mwanadamu uhalali wa kufanya vitu kwa niaba ya Mungu. Kuna vitu ambavyo
Mungu alitakiwa kufanya moja kwa moja kwenye maisha ya watu. Sasa ili kuwezesha
utekelezaji wa majukumu, amewapa
wanadamu tabia zake, ili wafanye kazi kama yeye, kwa niaba yake kwenye
maisha ya watu.
Kuna
tabia ambazo wanadamu wamezipoteza baada ya dhambi, na nyingine kwa uwezo wao
wa kibinadamu hawawezi kuwa nazo, lakini bado Mungu ametoa namna ya kuwasaidia
kuwa na tabia hizo ili wazidi kuwa na upana wa kutumiwa na yeye katika dunia
yao.
Mwanadamu
wa kawaida, ni ngumu kwake kuwa mtakatifu, lakini Mungu mwenyewe ametoa msaada
wake kwa njia hii kuwa mtu AMWAMINI YESU KRISTO kuwa alikufa msalabani kwa
ajili ya dhambi zake, kisha APOKEE KIPAWA CHA ROHO MTAKATIFU na kuamua
kuongozwa naye, na kuamua kuishi maisha ya haki yatokanayo na Neno la Mungu.
Hii inamsaidia mtu kuwa mtakatifu.
Na kuna
vitu kwa Mungu haviwezi kubebwa bila huyo anayebeba kuwa mtakatifu. Asipokuwa
mtakatifu, akibeba tu vitamuua. Kwahiyo, ili avibebe, Mungu anamsaidia kuwa
mtakatifu, kumbuka utakatibu ni tabia ya Mungu. Ni tabia inayomtafsiri Mungu na
namna anavyotofautishwa na miungu mingine yote, kwahiyo tabia hii mtu akiwa
nayo, kuna viwango vya kutumiwa na Mungu vinakuwa vikubwa sana kwa sababu tabia
ya kubeba hicho kiwango anayo.
Mfano wa
tabia nyingine ni upendo, Mungu ni pendo, hauwezi kumtenga Mungu na upendo. Na
mwanadamu wa kawaida upendo wake una walakini, ni jambo dogo sana kuacha
kumpenda mtu mwingine kwa sababu fulani fulani. Lakini Mungu ana upendo mkubwa
sana hata kwa watenda dhambi, hata kwao ameruhusu mwanae wa pekee afe msalabani
kwa ajili ya wote. Huu ni upendo uliovuka mipaka.
Hata
Yesu aliuonesha upendo huu kwa ukaribu wake na namna alivyoshughulika na dhambi
za makahaba, watoza ushuru na watu wa mataifa. Upendo ni tabia ya Mungu,
inayomfanya Mungu afanye vitu vingi kwenye maisha ya wanadamu bila kuchoka. Ili
mtu afanye kazi kwa niaba ya Mungu lazima awe na tabia hii ya Upendo. Mungu kwa
sababu anajua umuhimu wa tabia hii ya Upendo, anaijenga na kuimimina tabia hii
kwa njia ya Roho Mtakatifu ndani ya mtu.
Kwahiyo,
mtu anaweza kabisa kutumiwa na Mungu. Anaweza kumsaidia Mungu kugusa maisha ya
watu. Anaweza kufanya kazi na Mungu, kwa sababu alivyo yeye Mungu ndivyo na
mwanadamu anakuwa. Na haya yote yamewekwa wazi katika maandiko matakatifu ya
Biblia katika vitabu mbalimbali.
Unaweza
kushiriki tabia ya uungu wa Mungu. Unaweza kubeba tabia za Mungu, ambazo
zinakupa uhalali wa kutumiwa na Mungu. Hata kama kuna mtu unamuona hafai, huyo
anaweza kutumiwa na Mungu kama kuna baadhi ya tabia ambazo zimeharibiwa ndani
yake (kama kufikiri na maamuzi) zitaamshwa na kurudishwa kama awali Mungu
alivyokusudia, na kama atawezeshwa kupata asili ambazo zinatokana na utendaji
wa Roho Mtakatifu kwenye maisha ya mtu.
3.
Watu Wanaweza
Kuhusiana Na Watu
Mungu
amewaumba watu katika hali ya kutegemeana, watu wanaweza kuhusiana. Ndiyo maana
Mungu ana uwezo wa kumtumia mtu ili kumsaidia mtu mwingine hapa duniani. Kila
mwanadamu anamtegemea mwanadamu.
Tunawahitaji
watu maishani mwetu. Hakuna mtu ambaye hawezi kuwa na uhusiano mzuri na watu.
Hata kama aseme yeye ameumbwaje, kila unayemuona ameumbwa na Mungu, amewekewa
ndani yake uwezo na asili ya kuhusiana na wengine.
Mungu
hakuona kuwa ni vyema kumuacha Adamu peke yake, lakini ajabu ni kuwa Hawa
alitoka kwa Adamu, maana yake kuna kitu
ambacho Adamu atakipata kwa Hawa ndiyo maana ikalazimu uwepo wa Hawa.
Mtu
ambaye haheshimu uwepo wa watu wengine, anayejiona anajua vyote, ambaye hajali
wengine wala kuonesha upendo kwa walio dhaifu, anajaribu kumkosoa Mungu
aliyeweka asili ya kutegemeana baina ya mtu na mtu. Na ukweli ni kwamba
hatafika popote maishani.
Kuna
watu maishani wamepewa vitu ambavyo vitakusaidia wewe. Usipojua kuwa wana vitu,
unaweza kukaa kwenye maombi unasubiri vije, kumbe tayari vipo, ni kumuomba
Mungu hekima ya kuwajua watu na kuhusiana nao vyema.
Sauli
(Paulo) alitokewa na Yesu, lakini ajabu ni kuwa Yesu mwenyewe akamwambia aende
kwa Eleazari, na wakati Yesu mwenyewe angeweza kumwambia yote. Sasa kwanini
amwambie aende kwa mtu? Yesu hawezi kuvunja kanuni ambayo aliiweka tangu mwanzo
ili kuongoza maisha ya mwanadamu. Ameshaweka asili na kanuni ya kuhusiana,
hatafanya kazi na mtu mmoja, atafanya kazi na kila mtu, kwahiyo, mtu asije
akadhani peke yake ndiye anamjua Mungu kuliko wengine.
Hata
Paulo mwenyewe pamoja na kazi yake yote, lakini bado kuna vitu alienda kuuliza
kwa kina Petro. Hii ni asili ya wanadamu, haiwezi kukwepeka. Hata kama utaenda
maombi na kukaa milimani, kuna vitu tu utalazimika (kulazimishwa) kuja kutafuta
watu hata kama ulikuwa unawadharau na kuwaona kuwa hawafai.
Kuna
vitu Mungu huwa anawapa watu, na akishawapa watu, ni wajibu wa watu kwenda kwa
hao watu, na wanapaswa kwenda kwa msaada wa Mungu, kwa sababu kila mtu ambaye
kuna kitu amepewa kwa ajili yako, kuna majira yake kukipata kwake. Na kuna
hekima pia ya kupata hicho kitu kwake, hauendi kichwakichwa.
Mungu
anatumia watu kwa sababu ametengeneza uumbaji wote katika hali ya kutegemeana,
na hali hiyo haiwezi kuondoka. Ukielewa hili, itakusaidia sana kuona watu namna
ambavyo kuna vitu vingi wamebeba vya thamani sana kwa ajili yako, ni wewe tu
kukosa hekima ya kuhusiana nao.
Kila mtu
anamtegemea mtu mwingine. Hakuna kukwepa hili. Ukiona jambo hata Mungu mwenyewe
hakwepi jambo fulani, ni lazima ujue kuwa lina uzito kwake usio wa kawaida, na
ukitaka kutoboa unapaswa kulichukulia jambo hilo uzito ambao na yeye
anauchukulia.
Wakati
mwingine inahitaji kufunguliwa ufahamu kwa maombi, au kwa taarifa kama hizi,
ili kuelewa ulazima wa kuhusiana vizuri na watu maishani mwako. Siyo lazima
aletwe malaika Gabrieli, na wakati mwingine hata akija, bado atakuelekeza kwa
watu kama Mariamu alivyoelekezwa kwa Elizabeti.
4.
Watu Wamepewa
Mamlaka Juu Ya Nchi
Mara
baada ya Mungu kuiumba dunia (nchi), kisha akamweka mwanadamu, ni mwanadamu
pekee mwenye mamlaka na dunia. Ndiyo maana hata shetani alipotaka kuitawala
dunia, alienda kwanza kwa mwanadamu.
Duniani
hauruhisiwi kufanya chochote bila kuwepo kwa mwanadamu. Mwanadamu ndiye mwenye
maamuzi na dunia. Ni kweli kuwa Mungu ni muumbaji wa vyote, na anatawala vyote,
lakini akimpa mtu nafasi, haingilii nafasi hiyo mpaka huyo mtu amtengenezee
nafasi au kumpa nafasi Mungu aingilie kati katika jambo husika.
Inamlazimu
Mungu kufanya kazi na watu au kutumia watu kwa sababu hawezi kuvunja mfumo
aliouweka mwenyewe na akauainisha kwenye Neno lake. Yeye akiainisha kitu,
hakika anakilinda na kukiheshimu kwa sababu ya uaminifu wake. Inahitaji nafasi
ya watu kumpa Mungu nafasi ili afanye kazi duniani. Ndiyo maana Mungu anafanya
kazi na watu.
Kinachoruhusiwa
kufanya kazi kwenye dunia ni chenye mwili, ndiyo maana ililazimu hata shetani
aingie ndani ya nyoka, Mungu aongee kupitia punda ili kumjulisha vitu Balaamu.
Sasa hawa viumbe wengine wanatumika kwa dharura sana, asilimia kubwa sana
wanaotumika hapa ni wanadamu kwa sababu wanadamu ndio wenye mamlaka juu ya
viumbe wengine wote na kila kitu kinachofanyika.
Ni
ukweli kuwa ukimpata mwanadamu umeipata dunia. Mungu akimpata mwanadamu mmoja,
anaweza kuipata dunia nzima na kuisaidia katika jambo husika. Kutokana na
mamlaka aliyonayo mwanadamu, Mungu hakwepi umuhimu wa mwanadamu kwenye kufanya
kazi zake hapa duniani.
Ukielewa
hii utajifunza kuwa, hautatumika wewe peke yako. Mungu anamtumia mwanadamu
yeyote ambaye amempa yeye [Mungu] nafasi. Kwahiyo, ukiamua kumtengenezea Mungu
nafasi, ataonekana kwenye maisha ya watu na dunia nzima kupitia yeye.
Ndiyo
maana mahali fulani pameandikwa kuwa Mungu hafanyi jambo bila kuwajulisha
watumishi wake. Kwanini anawajulisha, ni kwa sababu anatafuta mlango, na wao
wakifungua, Mungu anaingia kazini kusaidia wanadamu.
Hata
wewe unaweza kumtengenezea Mungu nafasi ya kusaidia kizazi chako. Unaweza
kuanza hili kwa kuwekeza kwenye maombi na mifungo ya kumwambia Mungu kuwa
unahitaji kutumiwa na yeye kwa ajili ya utukufu wake, kuwekeza kwenye ufahamu
ambao unaamua upana ambao Mungu atafanya kazi na wewe, kutafuta kujua eneo gani
ambalo Mungu amekusudia kufanya kazi na wewe na kuwekeza hapo, na pia kukaa
chini ya watu wenye uzoefu wa maeneo mbalimbali ambayo Mungu amefanya nao kazi.
Ndugu
msomaji, usikubali kutokuwa sehemu ya watu ambao wanafungua mlango kwa yeye
kufanya kazi kupitia wao maishani. Amua leo, na chukua hatua madhubuti, na
maisha yako yatakuwa yenye tija. Na itakuwa vyema sana kama utawaisadia
wengine, kufungua mlango ili nao pia watumiwe na Mungu, maisha ya watu Yazidi
kujengwa katika wema kwa mapenzi ya Mungu mwenyewe.
5.
Ni Furaha
Ya Mungu Kufanya Kazi Na Wanadamu.
Mungu
anafurahia sana kufanya kazi na wanadamu. Mungu anajivunia sana kufanya kazi na
wanadamu. Ni fahari ya Mungu kufanya kazi na uumbaji wake kwa ajili ya uumbaji
wake. Inampa sana yeye utukufu.
Mungu
anafurahia kufanya kazi na wewe ili watu wengine wasaidike na maisha yao yajengwe.
Mungu anatamani sana kufanya kazi na wewe ili maisha ya watu yawe na tija hapa
duniani.
ni
furaha kwa sababu, hii inaonesha namna ambavyo uumbaji wake umekuwa na tija
mbele zake. Unaleta matokeo aliyokusudia huo uumbaji ulete. Mungu anafurahia
kufanya kazi na wewe kwa matokeo unayomletea.
Mungu ni
furaha yake kukupa ufalme, ili uende nao popote, na ulete matunda yanayoeleweka
mbele zake. Mungu anafurahi sana anapokuona unakuwa mtu mwenye tija kwenye
kizazi chako.
Jifunze
hili, Mungu hatafanya kazi na mtu mmoja tu peke yake, wakiwepo wengine,
watafanya naye kazi pia, maana wote ni uumbaji wa Mungu, na ni kawaida na
furaha ya Mungu kufanya kazi na uumbaji wake.
Mungu
anafurahi anapokuona amekutuma mahali, amekupa maelekezo, unaenda pale,
unafanya kama ulivyotakiwa kufanya, na unaleta mezani matokeo yaliyopangwa. Ni
jambo dogo sana yeye kukuamini katika yaliyo makubwa zaidi.
Mungu
anapofurahi, na wewe lazima uingie katika furaha yake. Hili linaelezwa katika
mfano wa watumwa waliopewa talanta na bwana wao wakazifanyie kazi, wale wote
waliokuja na kitu mezani, aliaambiwa vyema mtumwa mwema, ingia katika furaha
(raha) ya bwana wako. Mungu akifurahi, utashiriki furaha yake.
Kumbuka
kuwa FURAHA YA BWANA ndiyo nguvu yetu. Mungu akifurahi, maisha ya aliyechochea
furaha ya Mungu lazima yabadilike, inamfanya aaminiwe katika nguvu na hekima
nyingi zaidi, ili azidi kuwa na matokeo mbele za Mungu.
Ndugu
msomaji, hii ikupe shauku ya kumpendeza Bwana Mungu. Yeye amesema siyo wale
wamwitao Bwana Bwana ndiyo watakaourithi ufalme, ni wale wayafanyao mapenzi ya
Baba (Mungu). Wayafanyao mapenzi yake (matakwa yake) ndio wampendezao, na hao
ndio ambao atakuwa na furaha nao. Hao atawaongezea kicheko, na hawatakuwa
wanyonge katika kizazi chao.
Ndugu
msomaji, ni imani yangu kuwa katika somo hili umepata mambo mengi ya kukujenga,
na hakika maisha yako hatabaki kama yalivyo. Wikiendi hii ikazidi kuwa ya
baraka. Mwaka huu, azimia kufanya kazi na Mungu, na uwe mtu wa matokeo. Karibu
tena wikiendi nyingine.
Comments
Post a Comment
Thanks for your comment, God bless you!!!