MAAMUZI 5 YA KUFANYA KAMA UNATAKA KUFIKA MAHALI MAISHANI.

Ukweli ambao kila mtu anapaswa kujua kuwa, hakuna mtu aliyeumbwa ili kuwa asiye na kitu maishani, au mwingine kuwa na kitu maishani. Kila mwanadamu ambaye amezaliwa chini ya jua, anayo nafasi ya kuboresha maisha yake, bila kujali ametoka kwenye hali gani.

Tatizo siyo kuwa umezaliwa wapi na lini, tatizo lipo kwenye maamuzi yako ya sasa. Hakuna maana ya kulaumu watu, au viongozi au mifumo kila siku, na wakati unayo nafasi ya kuamua kufika mahali ambako Mungu amekusudia kukufikisha kama ukiamua kuanza.

Kila unayemuona amesimama mahali pa juu katika haki na kweli, amepitia mchakato, na hajafika pale kama bahati au ajali, aliamua kuwa pale alipo. Usipoamua, utaishia kuwa huyo ulivyo kila siku, na hali mbaya zaidi kwa wanaokuja baada yako.

Hauwezi kubadili walichofanya wa nyuma yako, lakini unaweza kubadili kuanzia hapo ulipo, na kwa ajili ya wale watakaokuja baada yako, ni aibu kubwa sana kuamua kutumia miaka yako yote duniani kuishia kulaumu watu, nchi, mifumo, na viongozi, na wakati wao wana akili kama wewe, mwili kama wewe, ni wanadamu kamili kama wewe na wana masaa 24.

Kila unayemuona amekuwa juu katika eneo fulani. Kuna maamuzi 5 aliyafanya, ambayo yamegeuza kabisa maisha yake. Hatahivyo, usidanganywe kuwa kuwa mtu fulani ni tukio la mara moja, pamoja na kuwa utashika hayo maamuzi, kutakuwa na mchakato wa muda fulani, utakaokutoa hatua mpaka hatua, ili ufike pale. Kufika mahali maishani, siyo jambo la siku moja, ni mchakato, ni safari inayohitaji kujikana, inayohitaji uvumilivu maana usipokuwa makini maamuzi yako mwenyewe utayatupa njiani na kuamua kufanya mambo ya kawaida, ambayo huwafanya watu kuishia kuwa wa kawaida tu maishani.

Karibu tujifunze maamuzi hayo.

 

1.     Amua kutafuta ufahamu wa kule unakohitajika kuwa kiasi kwamba akili yako imemezwa na kule unakohitajika kuwa.

Huwezi kufika mahali zaidi ya ufahamu wako ulivyo. Ukitaka kufika mahali hakikisha kuwa akili yako imefika hapo. Usichoweza kukimiliki kwa akili yako, kiasi kwamba akili yako imeshawishika na kuathiriwa nacho kiasi cha kubadili hadi mfumo wako wa kusema na kutenda, hauwezi kukimiliki mwilini.

Kila unayemuona amefanikiwa, amewekeza kwenye ufahamu wa kule anakotakiwa kuwa. Akifahamu kuwa anatakiwa kuwa mfanyabiashara, anawekeza katika ufahamu wa biashara, kwa kina, kiasi kwamba, maneno yake, na matendo yake, yanakuwa matokeo ya kile anachokifahamu kuhusu biashara au huko anakohitaji kuwa.

Kama usipofika kiwango ambacho unachosema, na unachofanya ni matokeo ya ufahamu wako juu ya kule unakohitajika kuwa, hautaweza kufika huko, asikudanganye mtu kuhusu bahati.

Mambo mengi ambayo Mungu alikuwa akiwafundisha wana wa Israeli jangwani, ilikuwa ni kwa ajili ya Kanaani. Wengi wao waliposhindwa kujenga ufahamu wao, waliishia jangwani.

Mungu hataruhusu kamwe, wewe ufike mahali ambako akili yako haiwezi kustahimili kuishi, maana anajua utakufa. Utabaki hapo ulipo, mpaka ukamate akili ya kule unakohitajika kwenda, la sivyo utabaki hapo hapo.

Usipokubali kulipa gharama ya kujifunza mambo ya kule unakohitaji kuwa, sahau kuwa kule unakohitajika kuwa. Ndiyo maana, watu wote waliofanikiwa unaowaona na kuwasoma kwenye habari mbalimbali, mojawapo ya siri wanayoishika kila siku ni KUJIFUNZA. Wanalipa gharama kujifunza, kuliko kitu kingine.

Ni wale tu wanaojiandaa kufa maskini, wasio na kitu, wasio na alama kwenye maisha ya watu, wasio na matokeo, wasio na faida duniani, ambao hawakubali kulipa gharama ya kujifunza.

Ukweli ni kwamba, kujifunza ni gharama, ndiyo maana wengi wanashindwa kujifunza, wanakuwa na visingizio vingi. Maarifa yanatafutwa, na yanakamatwa sana. Maandiko yanasema mkamate sana elimu. Unahitaji kukamata sana mafundisho ya kule unakotaka kuwa.

Wengi wetu wanasikiliza kila kitu, wako bize na tamthiliya, muvi, na mfululizo wa hadithi mbalimbali, na vitu vingine, ambavyo ukiwauliza vitakupeleka mahali unakohitaji kwenda, watakuambia hapana, na bahati mbaya wapo tu hapo hapo kila siku.

Ikiwa unahitaji kufika mahali maishani, amua kutafuta ufahamu wa huko, na kuhakikisha kuwa, umeathiriwa kabisa na ufahamu huo. Yaani imani yako imekomaa kabisa kiasi kwamba, unaona kabisa sehemu hiyo, kiasi cha kubadili mfumo wako wa matendo ili kuelekea sehemu hiyo. Inawezekana kama ukiamua.

 

2.    Amua kukaa chini ya malezi.

Huwezi kufika mahali maishani bila kukaa chini ya malezi. Asiyelelewa, ni chokoraa, hawezi kuwa chochote maishani. Ndiyo maana unaona kuna taasisi, zinawalea wale watoto wa mtaani waitwao machokoraa, kwanini wanawalea? Wanawapa malezi kwa sababu ni mtu anayekaa kwenye malezi tu ambaye atafika mahali maishani.

Wana wa Israeli ili kufika nchi ya Ahadi, iliwalazimu kukaa chini ya malezi ya Musa na baadaye Yoshua. Hautafika mahali bila kukaa chini ya malezi. Hauwezi kukwepa malezi kama unataka kuwa mtu maishani.

Usipokubali kuwa chini ya mtu fulani anayekuwajibisha, na kufuatilia ukuaji wako, ambaye anajua kabisa wapi unaelekea, na umepewa mtu huyo na Mungu mwenyewe, hautakuwa mtu katika dunia hii. Watu wengi wanajitafutia watu wao wawalee, ambao hawatawawajibisha kuwa bora, Mungu akupe mtu wa kukulea na kukuwajibisha.

Hii ni kanuni isiyokwepeka, hata kwa wale ambao wanatumia nguvu za giza kuendesha shughuli zao, wanalelewa na wakuu wao. Lazima uwe chini ya malezi. Hakuna mtu mkuu asiyekuwa chini ya mtu. Kila mkuu, ni mlelewa wa mtu fulani mkuu zaidi yake hata kama haujamuona huyo mkuu wake.

Hautakuwa chochote kama unajiamulia chochote, hakuna anayekuonya ukikosea, ukiamka na lolote, hilohilo ndiyo unalo. Hakuna mtu wa kukuonya, wewe unajua kila kitu. Yaani hata kama unajua vitu vyote, una kila kitu, na unatakiwa kufika mahali, kama haupo chini ya malezi, huko unakotaka kwenda utaishia kusikilizia kwenye masikio na ndoto za usiku tu.

Mungu hawezi kuruhusu mtu asiyewajibika kwa mtu fulani kuwajibika kwa ajili ya dunia au taifa. Huyu mtu ni sekunde chache kuwa na kiburi, ni sekunde chache kufanya maamuzi ya hovyo ambayo yataharibu maisha ya wengi. Ndiyo maana hata kina Daudi walikuwa chini ya walezi kama kina Nathani nabii. Siku sauli alipodharau nafasi ya Mlezi wake Sauli, na kuona kuwa nafasi ya ufalme ni kubwa kuliko ya mlezi, ndiyo siku ambayo, Mungu aligeuka na kumuacha, akaenda kutafuta mtu mwingine aitwaye Daudi.

Anayekaa chini ya malezi kwa uaminifu, anaupendeza moyo wa Mungu, na ni rahisi kuaminiwa na Mungu katika vitu vya Mungu katika sehemu fulani. Kama kweli, moyoni mwako, unajua kuwa Mungu anakuita kuwa mtu fulani hapa duniani, badi amua kumtafuta Mungu akuweke chini ya malezi ya mtu fulani, na ufanye hivyo, na uwe mwaminifu hapo

 

3.    Amua kutunza na kulinda nafasi ya Mungu maishani mwako.

Kila unayemuona amekaa kwneye kitu fulani kwa haki na kweli, amewekwa na Mungu, na wakati mwingine hata wabaya wameruhusiwa kwa ajili ya ajenda fulani maalumu.

Mungu hatakuweka juu kama haujajifunza kutunza, kulinda na kuheshimu nafasi yake kwenye maisha yako. Watu wengi wanatafuta kuwa watu fulani, halafu wanasahau kabisa kulinda nafasi ya Mungu kwenye maisha yao.

Ukweli ni kwamba, unamhitaji Mungu kuliko unavyodhani ndugu yangu. Hata kama unajihisi una uwezo kiasi gani, una nguvu, una fedha, una hekima, ukimkosa Mungu hautafika popote. Ndiyo maana kuna watu inaonekana wana kila sababu ya kuwa mahali fulani, lakini hawajawahi kuwa hapo, hii hutokea kwa sababu Mungu hajapewa nafasi anayostahili katika maisha ya huyo mtu.

Kuna mtu ukimsikiliza, unaona kabisa kuwa ana kitu, na ana uwezo. Lakini tatizo, mbona kila siku yuko hapo hapo, anapambana lakini hasogei. Ukiona haya, ujue tu kuwa huyo mtu ameamua kwenda mwenyewe bila Mungu.

Kila wakati ambao wana wa Israeli walisahau kutunza na kulinda nafasi ya Mungu kwenye maisha yao, mambo yao yaliharibika, na wengine walikufa jangwani kabisa. Ukishindwa kutunza nafasi ya Mungu, huwezi kutunza nafasi utakayopewa huko juu.

Mungu anawapandisha juu wale wanaolinda nafasi yake kwenye maisha yao. Yusufu alikubali hata kwenda gerezani kwa kesi ya kulazimishiwa ya kumbaka mke wa mkuu wa kitengo cha ulinzi ili tu asimkose Mungu. Alichokuwa analinda hapa ni nafasi ya Mungu kwenye maisha yake.  Na tunafahamu kuwa hii ilimfanya awe mkuu katika taifa alilopelekwa hata kama ni ugenini.

Haitoshi kuota ndoto, Yusufu aliota ndoto, alijua kuna mahali anaenda, lakini alihakikisha analinda nafasi ya Mungu. Tunajifunza hili pia kwa Danieli, huyu alisimama imara kwenye kulinda nafasi ya Mungu, na tunaona namna ambavyo aliinuliwa juu zaidi ya wengine bila kujali alikuwa ni mgeni.

Wengi wanacheza na dhambi, halafu wanataka kufika mahali. Wanafanya kila aina ya uchafu. Dhambi nyingine wanazifanya kwa siri, wakidhani kuwa wanafanya kifichoni, kumbe wanafanya mbele za Mungu, na Mungu akiwaangalia, anageuza uso wake kwao, na wanaishia kutokuwa chochote.

Usipoazimia kuwa mtakatifu kweli kweli na kujitenga na dhambi. Usipoamua kuishi chini ya uongozi wa Roho Mtakatifu na maelekezo yake. Usipoamua kumuomba Mungu msaada wa kukusaidia kuwa mtakatifu kama yeye alivyo Mtakatifu. Usipoamua kuwa mtu wa ibada ya kweli. Usipoamua kuwa mtoaji kwa moyo mweupe na wa kweli. Usipoamua kuyatoa maisha yako kwa Mungu, hautafika popote maishani.

 

 

4.    Amua kuishi kwa tabia zinazoeleweka ambazo utaziishi ukiwa kule juu.

Mungu mwenyewe, hakuwa anawapa sheria wana wa Israeli jangwani kwa ajili ya jangwani, alikuwa anawapa kwa ajili ya wao kuziishi kule Kanaani. Wakishindwa kuziishi wakiwa jangwani, hawawezi kuziishi wakiwa nchi ya Kanaani.

Kama usipokubali leo kuanza kuishi kanuni ambazo utaziishi kule juu, usiweke kabisa kichwani mwako kuwa utaishi kule juu. Haipo hiyo kabisa.

Kama unajua kule juu panahitaji uaminifu, na wewe haujifunzi na kuiishi katika uaminifu sasahivi, kamwe hautakuwa pale juu. Kama ukijua kule kunahitaji watu wenye nidhamu na muda, na usiwe na maisha ya nidhamu sasa hivi, hautakuwa chochote.

Kule juu hakuhitaji watu wanaolala masaa mengi, watu wavivu, wasio na bidii, wasio na maadili, watu wasiofanya kazi zinazoeleweka. Kule juu watu wenye bidii ndiyo wanaopata nafasi.

Kama usipoanza leo kuishi maisha ya bidii, ya utendaji kazi wenye akili, usitegemee kufanya hivyo ukiwa kule. Haiwezekani ndugu yangu.

Maisha ni utaratibu unaopangiliwa, usipojifunza kupangilia leo matumizi ya muda, matumizi ya fedha, na rasilimali nyingine, hautajifunza kufanya hivyo siku ukiinuliwa, ndiyo maana wengi wana vitu lakini hawainuliwi na bado wapo hapo kila siku.

Tabia yako inaamua utakuwa wapi kesho. Kama tabia yako ni ya hovyo, utaishia kukaa mahali pa hovyo siku zote. Amua kujenga tabia yako leo.

Kama leo hauwezi kusimamia hisia zako, unaendeshwa na kemikali za mwili. Usitegemee kuwa ukioa au ukiolewa utaweza kusimamia, badala yake zitazidi kukuendesha.

Usichoweza kukitawala sasahivi, huwezi kukitawala ukiwa juu. Kama unahitaji kufika kule juu, jifunze tabia za kule juu, na anza kuziishi leo.

Hatahivyo, hii isikufanye kuishi nje ya uwezo wako wa sasa, ninapomaanisha tabia, nalenga zaidi kwenye nidhamu ya maisha kwa ujumla. Mfano kuhusu fedha, kama usipojifunza kutumia fedha kwa nidhamu sasahivi, hautatumia kwa nidhamu kesho.

Kama hauwezi kuweka akiba, au kuwekeza, hata kesho hautawekeza kwa sababu hauna huo msingi. Kumbuka maisha ya watu yanaamuliwa na misingi iliyojengwa tangu huko nyuma.

Kila unayemuona leo, ni matokeo ya misingi yake aliyoiweka au kuwekewa jana. Maisha na nafasi maishani si ajali. Misingi mizuri itakupa nafasi nzuri na maisha mazuri.

Usipoamua kuwa mtu wa mipango na tathmini leo, usidhani kuwa kesho utakuwa mtu wa mipango na tathmini. Usipokuwa mtu wa maombi leo, kesho kule juu hautakuwa hivyo, na kwa sababu hiyo, haupaswi kuwa pale juu. Amua leo kujenga tabia yako.

 

5.    Amua kufanya kazi na watu sahihi.

Ukweli ni kwamba, hautafanya kila kitu peke yako. Unahitaji kufanya kazi na watu ili ufike juu. Hata Musa alifanya kazi na Haruni, Miriamu, Yoshua, Huri, Kalebu na wazee na wengine.

Kila aliyepo juu, kuna watu ameinuka nao, ambao anafanya nao kazi pale. Na uwe na uhakika kuwa hao watu, ameanza nao huko nyuma.

Siyo kila mtu unapaswa kufanya naye kazi hata kama unahisi unampenda. Wengine unapaswa kuwaweka pembeni. Hatufanyi kazi na watu kwa sababu tu tunawapenda, tunafanya nao kazi kwa sababu ni watu sahihi.

Hakikisha unazungukwa na watu sahihi, ambao watakuchochea na kukuhimiza na kukufanya kila siku uwe na nguvu ya kuendelea mbele. Mungu anafanya kazi na watu, ukiwa na watu sahihi itakusaidia sana.

Usikubali kufanya kila kitu peke yako, hata kama unaona kuwa unaweza kufanya, shirikisha watu ambao Mungu anakupa. Hii itakufikisha mbali.

Kuna msemo usemao kuwa ukitaka kufika haraka, nenda peke yako, ila ukitaka kufika mbali, nenda na watu. Msemo huu ni wa kweli kabisa. Umbali na nafasi unayofanya, huamuliwa na watu unaofanya nao kazi.

Yesu kuwa na kazi ambao inadumu mpaka leo, ni matokeo ya watu aliofanya nao kazi hata kabla hajaondoka duniani. Ameondoka, lakini bado kazi ipo kwa sababu kuna watu kadhaa aliamua kufanya nao kazi.

Anza pale ulipo, na watu wale ambao utaanza nao, usisubiri liwe kundi kubwa sana, anza vile ulivyo na wale ulionao na taratibu kadri unavoendelea kuwa mwaminifu katika madogo, ndivyo unavyoaminiwa katika makubwa zaidi.

Ukiweza kwenda na hao ulionao, ni rahisi kwenda na wengine utakaoongezewa.

Ndugu msomaji, mambo haya 5 ni maamuzi ambayo kila mtu mkuu aliamua kuyafanya, ndiyo maana unamuona pale alipo. Mahali na nafasi fulani maishani si ajali, ni matokeo ya maamuzi yaliyofuatwa kikamilifu kwa muda fulani. Unaweza kuwa yule unayepaswa kuwa, kama utaamua kulipa gharama hiyo leo.

Mungu akubariki.

Comments