Ndugu msomaji karibu katika wikiendi nyingine njema na ya baraka sana. Natumaini kuwa wiki yako imeenda vizuri na Mungu amekulinda.
Leo tunajifunza juu ya mambo 7
ya kutusaidia kuwa na alama kwenye maisha ya watu. Kuwa na alama kwenye maisha
ya watu, ni kufanya mambo ambayo kwa namna moja ama nyingine yanaongeza thamani
ya maisha ya watu wengine, na kuwafanya wawe bora kuliko walivyokuwa jana. Kuwa
alama kwa lugha nyingine ni kuwa kielelezo kwenye maisha ya watu, kuwa mtu
ambaye wengine wanajifunza na kupata picha ya wanavyotakiwa kuwa.
Karibu tujifunze mambo haya
1.
Nidhamu Binafsi
Hili ni jambo la kwanza la
kuzingatia kama unahitaji kuwa na alama kwenye maisha ya watu. Kama unahitaji
kuwa na nafasi kwenye maisha ya watu, na kuwa kielelezo chema kinachoongeza
thamani ya watu unahitaji kuwa na nidhamu binafsi.
Nidhamu binafsi inajumuisha
mfumo wa kanuni na taratibu ambazo umeamua kwa hiyari yako mwenyewe, umeweka na
kuamua kwenda nazo maishani ili kuamua utambulisho wako. Inamuisha mipaka
uliyojiwekea na namna unavyojichukua kwenye shughuli zako zote.
Nidhamu binafsi inahusisha
maamuzi ya makusudi kabisa, ya kuamua kuishi vyema na watu, sawasawa na kanuni
za MUNGU ambazo zinaendesha maisha ya watu.
Nidhamu binafsi inajumuisha
namna ambavyo unasimamia matumizi ya rasilimali zako. Unatumia muda kwa
mpangilio, unatumia fedha na vitu vyote ulivyoaminiwa na Mungu kwa faida. Wewe ni
mtunzaji. Haupotezi muda wako.
Unalinda muda kwa sababu unajua
maisha yako yamefungwa katika muda, na hakuna jambo ambalo utafanya nje ya muda
ukiwa hapa duniani. Kwahiyo, watu watakutazama kama mtu ambaye anatumia muda
wake ipasavyo, wanaweza kuapata kwake hekima nzuri ya kutumia muda na
rasilimali nyingine.
2.
Malengo Yanayofanyiwa
Kazi
Hili ni jambo la pili, ambalo
litakufanya uwe na alama au nafasi katika maisha ya watu. Kila mtu unayemuona
ambaye ameacha alama, au hata sasa bila kujali yupo hai, amekuwa alama
isiyofutika kwenye maisha ya watu, anaishi kwa malengo na yanafanyiwa kazi.
Kwenye hii dunia, hauwezi kuwa
na alama kwenye maisha ya watu, kama utaishi kiholela bila mpangilio. Maisha yasiyo
na mipangilio, hayawezi kutumika kuacha alama yenye tija kwenye maisha ya mtu. Wala
hayawezi kutumika kuwa mfano wa maendeleo ya watu katika jambo husika.
Unapaswa kuwa mtu wa malengo na
mikakati, uwe mtu ambaye unafanyia kazi. Haitoshi kusema una malengo, haitoshi
kuandika malengo, kama haufanyii kazi malengo yako, hautakuwa na tija katika
jamii yako wala dunia yako. Hakuna atakayefaidika na uwepo wako, hakutakuwapo
na kumbukumbu lako uondokapo duniani, na wala huko uendako. Inahitaji kuwa mtu
wa malengo.
3.
Mtazamo Chanya
Kuhusu Maisha
Kila unayemuona duniani, ana
mtazamo fulani kuhusu maisha, na mtazamo huo ndio unaomfanya awe mtu fulani
katika dunia yake.
Ni ukweli kwamba, kila
unachokifanya, namna unavyoongea, unavyoitikia mambo katika maisha, ni matokeo
ya mtazamo au mitazamo uliyonayo katika jambo husika. Kwahiyo, kama usipokuwa
na mitazamo sahihi, hautakuwa na jambo sahihi unalolifanya kwenye maisha ya
watu, na usiwe na alama yoyote kwa watu.
Unahitaji kufanya maamuzi ya
kuacha mitazamo ya kizamani ambayo ni mibovu, mitazamo yoyote isiyofaa,
mitazamo yoyote isiyokusaidia. Na hii inatokana na namna ambavyo kila siku
unalipa gharama kujifunza vitu chanya.
Kwa maneno mengine, unapaswa
kuangalia aina ya taarifa ambazo kila siku unajilisha. Hakikisha kuwa
unajilisha taarifa chanya maishani. Epuka taarifa ambazo zitakupelekea ufanye
vitu visivyo na tija na mwisho wa siku kuharibu nafasi yako kati ya watu.
4.
Ushirika
Wako Na Mungu
Hili ni jambo la nne la muhimu
sana kuzingatia kama unahitaji kuwa na alama kwenye maisha ya watu. Mungu huvuta
watu kuja kwetu ili tuwaachie alama isiyofutika ambayo itakuw ana tija kwenye
maisha yao.
Ukishindwa kuwa na ushirika
mzuri na Mungu, yeye hatakuruhusu uwe na nafasi kwenye maisha ya watu, kwa
sababu utaishia kuwa mharibifu wa maisha ya watu. Unahitaji kujenga na kulinda
na kuukuza ushirika wako na Mungu kila wakati.
Ni lazima ujenge tabia ya maombi
yasiyokoma, utakatifu, kujifunza Neno la Mungu kwa kina, kumtumikia Mungu kwa
dhati. Ni jambo dogo sana kwa Mungu kukuletea watu maishani ili uwasaidie kama
amekuona kuwa unamfaa.
Unamhitaji sana Mungu kuliko
unavyodhani kama unataka kuwa na alama isiyofutika kwenye maisha ya watu. Ni muhimu
kujua katika mchakato wa kusaidia watu, kuna wakati watu hao hao watageuka na
kufanya vitu usivyotarajia, inahitaji neema ya Mungu kuendelea kuwasaidia yaani
kutolipa mabaya kwa watu wakati wamefanya mabaya kwako.
Ukipuuzia nafasi ya Mungu kwako,
utatumia nguvu nyingi sana kuacha alama kwa watu. Utatumia sana nguvu kuishi na
watu vizuri. Unapaswa kufanya maamuzi ya kulinda na kuheshimu mahusiano yako na
Mungu siku zote. Mungu ni namba moja.
5.
Kuthamini
Watu
Hakuna mtu atakayempa mtu nafasi
ya kuacha alama kwenye maisha yake, kama mtu huyo haoneshi thamani kwake. Inahitaji
kuthamini watu ili kuwa na alama kwenye maisha ya watu.
Waone watu kwenye jicho la
kiungu. Kuna namna Mungu anawatazama watu kwa uthamani mkubwa sana kiasi
kwamba, akamtoa mwanae wa pekee ili kupitia yeye watu waokolewe. Thamani ya
mwanadamu ni kubwa sana mbele za Mungu.
Kimsingi, kuna ufahamu ambao
Mungu anao kuhusu watu, ambao sisi wanadamu hatuna kuhusu wanadamu wengine,
inahitaji kupata ufahamu huo, ili kuona thamani ya watu hata wakati ambao kwa
macho ya kawaida, wanaonekana siyo kitu chochote popote.
Unahitaji kufahamu kuwa kila mtu
ana kitu anaweza kufanya, kuna mahali akiwekwa anaweza kufanya maajabu, ni vile
pale alipo hajakutana na mazingira sahihi, watu sahihi na labda kuna ufahamu
ameukosa. Unapaswa kufanyika daraja la mtu kupata vile ambavyo akivipata,
vitasaidia kufunua thamani yake iliyofichika.
6.
Maono Yanayokimbiziwa
Kumbuka kuwa kila mtu anapaswa
kuwa na kitu anachokikimbizia kwenye maisha. Unapaswa kuwa na maono ambayo
unayafanya, unayafuatia kila siku na unahakikisha kuwa unasogea hatua moja
zaidi. Maono uliyonayo yanahusisha watu.
Kila mtu mwenye maono, anagusa
maisha ya watu. Iwe ni maono katika biashara, huduma, uchumi na mengine mengi. Kila
maono yanahusu watu na yanafanywa na watu.
Ikiwa una maono ambayo
unayafuatia. Ambayo yanakufanya uamke asubuhi na kuchukua hatua mbalimbali,
hakika utakuwa na alama kwenye maisha ya watu. Ni lazima uamue kuyakimbizia
maono.
Maono yanazaliwa na Mungu
mwenyewe ndani ya mtu kwa mtu anayetokana na Mungu na yanatoka kwa shetani kwa
mtu anayetokana na shetani.
Kila maono yamebeba ajenda
fulani katika ulimwengu wa roho kuhusu maisha ya watu. Ajenda hiyo inaweza kuwa
ya kwa Mungu au kwa shetani. Ukiamua kuwa na ukaribu na Mungu, utakuwa na maono
ambayo yanahusu maisha ya watu, ambayo yamebeba ajenda ya Mungu na siku zote
ajenda ya Mungu lazima iyafanye maisha ya watu kuwa chanya.
Ukitaka kuwa na alama kwenye
maisha ya watu, hakikisha una maono unayoyapambania. Yanayokuweka bize kila
siku. Yanayokupa sababu ya kuamka, na ulazima wa MUNGU kukulinda zaidi.
7.
Maamuzi Thabiti
Kila kitu maishani kinazaliwa
kwa maamuzi. Hauwezi kuwa na alama kwenye maisha ya watu, au katika dunia yako
kama haujafanya maamuzi thabiti. Ni ukweli kuwa kuna mambo utalazimika kuacha
hata kama ulikuwa unapenda kuyafanya, hata kama unahisi ni ngumu kuacha, hata
kama unaona hauwezi. Unapaswa kufanya maamuzi ya kuacha na Mungu hauyupo mbali,
usisahau kumpa nafasi akusaidie.
Ni lazima ufanye maamuzi ya
kujenga thamani yako, kwa sababu hauwezi kujenga thamani za watu wengine na
kuweka alama kwenye maisha ya watu, kama hata thamani yako umeshindwa kuijenga.
Huwezi kupenda wengine kiwango ambacho haujipendi.
Ni lazima kuamua kujifunza mambo
mapya, hata kama inaumiza na kuona kuwa ni uzoefu mpya. Kuacha alama au kuweka
alama kwenye maisha ya watu ni gharama. Hakuna bahati wala ndoto katika kuwa na
alama kwenye maisha ya watu. Ni maamuzi ya kulipa gharama.
Ni lazima ufanye maamuzi ya
kuwatumikia watu kwa niaba ya Mungu. Uwe tayari kutafuta mapenzi ya Mungu kwa
ajili ya watu, ili uwape watu kitu wanachohitaji hasa maishani. Kila kitu ni
maamuzi kwa sababu lazima kilipiwe gharama.
Kuna marafiki itakulazimu
kuachana nao, na kuna watu itakulazimu kujiweka karibu nao kwa maelekezo ya
MUNGU. Unahitaji kuamua kwa kweli.
Ndugu msomaji, ni ushauri wangu
kwako kuwa, kwenye maisha unapaswa kufanya maamuzi. Mwaka huu amua kuwa mtu
mwenye tija kwenye dunia yako na kizazi chako. Amua kulipa gharama. Amua kuchukua
hatua, amua kuwa mtu mwingine.
Ndugu msomaji, imetosha
kuendelea kuwa yule yule asiye na matokeo kila siku. Itoshe kuwa yule yule
ambaye jamii yake inamuona hana tija, wengine wanamuona hana kitu cha kuipa
dunia yake cha kufaa. Amua kuifunua hazina ambayo Mungu ameiweka ndani yako kwa
ajili ya dunia.
Ndugu msomaji, unapomaliza
wikiendi hii, amua kuzungumza na Mungu juu ya hili, muombe akusaidie na kukugeuza
kuwa mtu mwingine, utakayeifaa jamii yako. Ni matumaini yangu kuwa kuna siku
utanitumia ujumbe wa mabadiliko kutokana na Makala hii.
Nikutakie wikiendi njema, na
Mungu akubariki sana, tukutane wikiendi nyingine.
Comments
Post a Comment
Thanks for your comment, God bless you!!!