Ndugu msomaji, natumaini unaendelea vyema na maisha yako ya kila siku, na ninamshukuru Mungu ambaye amekuweka kuwa hai hadi sasa. Ni dhahiri kuwa ana mpango kamili na wewe, na anaona kuna nafasi ambayo bado unahitajika katika dunia yako. Na inawezekana hujaanza bado kufanya au unafanya, lakini hii ikutie moyo kuwa unapaswa kuendelea kufanya vitu ambavyo Mungu anafurahia ufanye.
Katika wikiendi ya leo, kama
ilivyo dhamira yetu kuwa ni kukuongezea thamani kila wikiendi ili uweze kuwa na
wikiendi ya thamani zaidi na kuboresha maisha yako, tutajifunza juu ya mtu
unayepaswa kuwa ikiwa unahitaji kutazamwa miaka michache ijayo katika taifa la
Tanzania.
Ndugu msomaji, ninaomba ufahamu
kuwa, miaka kadhaa ijayo, kuna watu ambao Mungu atawahitaji zaidi kwenye nafasi
mbalimbali ili watazamwe na watu. Ninapozungumza kutazamwa na watu, ninamaanisha
kuwa Mungu anakuweka ili uwe msaada kwa watu kupitia nafasi fulani.
Sasa, miaka kadhaa ijayo, siyo
kila mtu ataweza kupata nafasi ya kutazamwa na watu. Mungu hataruhusu hili. Kwa
sababu kuna aina ya watu anawaandaa ambao watafaa katika hiyo nafasi. Unapofika
wakati kama huo, siyo kila mtu atakaa, ni yule tu aliyeandaliwa.
Majira haya, ni majira ambayo
Mungu anamuandaa Daudi, japokuwa Sauli yupo kwenye kiti anatawala. Mungu
hatishwi na utawala wa shauri kwa sasa, kwa sababu kijana wake Daudi yupo
katika pango la Adulamu, na watu mia nne, ambao na wao wana hali mbaya, lakini
wanatengenezwa kwa ajili ya nafasi mbalimbali, na Daudi ni jemedari wao, ili
siku akipewa nchi, basi wao washike vitengo.
Mtu wa Mungu, hii nchi inaenda
kukabidhiwa kwa watu walioandaliwa tu na siyo vinginevyo. Hata kama ulikuwa
umepewa maono au unabii kuwa utakuwa na nafasi katika taifa, kama usipoandaliwa,
hakuna kitu utakachokuwa nacho kwenye taifa lako la Tanzania. Kwahiyo, haitoshi
wewe kuwa tu na maono ambayo unaweza kuwa umeyaandika kabisa, unapaswa
kuandaliwa. Daudi alipakwa mafuta ya kuwa mfalme, akiwa kijana fulani, lakini
alimchukua kukaa mapangoni huko Adulamu ili aweze kuandaliwa kwa ajili ya hiyo
nafasi. Haitoshi kuombewa, au kuwekewa mikono, au kupakwa mafuta na kuwekwa
wakfu kwa ajili ya taifa la Tanzania. Kama haujatengenezwa, hatutapewa
chochote. Rudi katika pango la Adulamu, huko utengenezwe na wengine, na
uhakikishe kuwa ukipewa nafasi, ukitazamwa MUNGU WAKO ALIYEKUWEKA ANAONEKANA NA
SI VINGINEVYO.
Sasa watu hawa walioandaliwa au
kutengenezwa ndiyo watu watakaokuwa na kipaumbele siku chache zijazo, nazo
hazitakawia. Mtu huyu ndiye atakayetazamwa na watu katika taifa lake.
Mtu huyu atatazamwa na wengi;
1.
Mtu
aliyeamua kuacha dhambi na kuwa mtakatifu kweli kweli
Hiki ni kitu cha kwanza kabisa,
kinachomjenga mtu ambaye atatazamwa na wengi katika siku chache zijazo kwenye
taifa la Tanzania. Mungu ni mtakatifu na anafanya kazi katika utakatifu na
anayefanya naye kazi lazima awe na tabia kama ya kwake, ambayo ni UTAKATIFU.
Kumbuka unapopewa nafasi,
unapewa na Mungu, na kama unapewa na Mungu, ni Mungu anayetaka kuonekana
katikati ya watu kupitia nafasi hiyo. Sasa, mtu ambaye si mtakatifu, hawezi
kumfunua Mungu aliye Mtakatifu. Yaani mwizi, hawezi kumuwakilisha mtu ambaye si
mwizi.
Ni jambo la kufahamu kwa upana
kuwa, tunapaswa kuwa watakatifu ili kumfunua Mungu aliye mtakatifu. Na
utakatifu hauigizwi, na siyo wa vipindi, na hautafutwi siku unapewa nafasi.
Kama hauwezi kuwa mtakatifu leo na kuufanya utakatifu kuwa maisha yako ya kila
siku, nikuhakikishie kuwa, hata kama uliombewa hautakuwa na nafasi.
Yusufu alipewa ndoto na Mungu,
kuwa atakuwa mtu mkuu kati ya nduguze, lakini alilinda utakatifu wake,
hakukubali kuchezea nafasi ya Mungu kwenye maisha yake. Kulinda utakatifu ni
kulinda nafasi ya Mungu kwako wewe ambaye unakusudiwa kupewa nafasi fulani
kwenye taifa miaka kadhaa ijayo. Potifa pamoja na cheo chake, na ushawishi
wake, na kila kitu alichokuwa nacho, bado hakuweza kabisa kuzuia utakatifu wa
Yusufu kubaki pale pale.
Mtu wa Mungu, kama umewahi
kuwaza, au umewahi kuona maono au ndoto, au umewekewa mikono na maombi, kuwa
utakuwa mtu fulani wa kutazamwa na wengi basi mojawapo ya jambo unalopaswa
kuliweka kipaumbele ni UTAKATIFU. Kwako utakatifu siyo ombi, ni lazima.
2.
Mtu
aliyejijenga kimaadili kiasi cha kuweza kusimama imara dhidi ya uharibifu
wowote kwenye nafasi husika.
Mtu wa Mungu ninatamani ufahamu
kuwa, kila nafasi unayoiona mtu amekalia, ina mambo yake, na kuna watu walianza
vyema lakini mwisho wa siku, kwenye nafasi hizo hizo wakaharibika, ni rahisi
sana kupata uharibifu kwenye nafasi.
Kama haujajijenga kimaadili
mapema, ile nafasi kutokana na mambo mengi yaliyopo, na namna ambavyo
itaonekana umepata mamlaka fulani, unaweza kufanya mambo ya hovyo, ambayo hata
wewe mwenyewe utajiuliza siku ukitoka kwenye hiyo nafasi.
Ninaomba kukusemesha jambo moja,
wale ambao unawalaumu kuwa wameharibika, na wanafanya mabaya pale kwenye kiti,
ni matokeo ya kutojijenga kimaadili kwa kina kiasi cha kutoshea mambo makubwa
na magumu na ya kutisha yaliyopo kwenye nafasi hiyo.
Ndugu yangu, ni bora utumie miaka
hata 30 kujijenga kimaadili vya kutosha ili kuja kufanya kazi kwa miaka 3
ambayo itadumu milele kama ilivyokuwa kwa Yesu, kuliko kuwa na maadili sifuri
yaliyojengwa kwa miaka mitatu, halafu ukae kwenye kiti miaka 30. Kwa sababu
maadili yako, ndiyo mizizi yako.
Kama maadili yako, ndiyo mizizi
yako, basi kadri ambavyo unajijenga kimaadili ndivyo ambavyo unazidi kupeleka
mizizi yako chini, hivyo hata ukipewa nafasi sitakupoteza kwa sababu msingi
wako una kina. Haupaswi kuwa na maadili ya nyanya, ambayo haina misingi ya kina
yaani mizizi iliyoenda chini sana, kiasi kwamba, ikianza kuzaa matunda yake,
lazima kuwe na mti pembeni unaoupa nguvu, nje ya hapo hamna kitu. Jifunze kuwa
kama mbuyu, hata kama umebeba matunda mangapi, lakini bado uko imara.
Hatari kuu katika nafasi ambazo
Mungu anawaweka watu ni kuwa, nafasi hiyo hiyo ndiyo inayoweza kukua kabisa.
Inawezekana kabla hujapewa nafasi unaonekana uko salama, lakini siku ukipewa
nafasi, ndiyo itajulikana umeharibika kiasi gani, na kifo chako kitakuwaje.
Ndivyo ilivyokuwa kwa Sauli,
mwanzoni alionekana afaaye sana, tena akakomesha uwepo wa waganga na wachawi
katika taifa, tena akaonekana kuwa anafanya sawasawa na mapenzi ya Mungu,
lakini baada ya muda, kiti kikamgeuza ghafla akawa mtu wa hovyo kiasi cha
kukataliwa na Mungu.
Ndugu yangu, unapaswa kujenga maadili
yako. Maandiko yanasema, aliyepaa kwenda juu zaidi, ndiye aliyeshuka chini
zaidi katika pande za chini za nchi. Kama kweli, ndani yako una mzigo, una
moto, una kiu na shauku ya kulitumikia taifa hili katika miaka michache ijayo,
basi hakikisha unajenga maadili yako sana.
Jifunze maadili ya kule unataka
kwenda, na uyaishi hayo, nje ya hapo hakuna nafasi utakayokuwa nayo. Hii ni kwa
sababu, watu wengi wameshapewa nafasi, lakini wakafanya mqambo ya hovyo, nje ya
matarajio, sasa Mungu anatengeneza watu wake, kama uko tayari, nenda
ukatengenezwe, ili miaka michache ijayo, ulifae taifa la Tanzania.
3.
Mtu
mwenye moyo uliopondeka
Hii
ni sehemu ya tatu inayomjenga mtu ambaye atatazamwa na wengi katika nafasi
fulani kwenye taifa la Tanzania miaka michache ijayo. Lazima awe na moyo
uliopondeka. Moyo ambao unampa Mungu nafasi ya kudhihirika na kufunua utukufu
wake katika taifa la Tanzania.
Ndugu
yangu, taifa la Tanzania halihitaji yeyote, limeshawahi kuwa na watu wenye
mioyo yenye kiburi, ambao walifanya walichojisikia wao, ambao walijiona wao
ndio miungu wa taifa hili, walifanya chochote walichofanya kwa sababu ya
mamlaka yao, sasa wanatafutwa watu wenye mioyo iliyopondeka.
Mtu
mwenye moyo uliopondeka, ndiye ambaye anaweza kufanya kazi na Mungu. Anaweza
kumpa Mungu nafasi akafanya kazi kupitia yeye, yuko tayari kushuka na
kunyenyeke mbele za Mungu, hatakuwa kama Sauli ambaye alitaka hata kumnyamazisha
Samweli aliyekuwa mwakilishi wa Mungu kwake.
Mwenye
moyo uliopondeka anafundishika. Ana moyo wa toba, akifanya makossa, anarudi
haraka kwa Mungu, na yupo tayari kupokea maonyo na kubadilika. Ndiyo maana
Mungu alimpenda Daudi. Daudi alikuwa na moyo uliopondeka, yeye hakujivunia cheo
chake, yeye hakujivunia mali alizopewa na Mungu wala mamlaka yeyote, siku zote
alinyenyekea kwa Mungu, na kwa watumishi wengine ambao Mungu amewaweka kwenye
taifa lake.
Ukiona
mtu anapita njia yake mwenyewe, hafundishiki, haonyeki, hakubali kuwa amekosea,
na kukubali kubadilika. Ukijaribu kumsahihisha anakutishia kuwa yeye amepewa
nafasi na Mungu, mara ameitwa, mara ana macho ya kiroho kuliko wewe, mara
anajua kuliko wewe, ujue huyo mtu hata kama anaomba sana, hatatumiwa na Mungu
kwa ajili ya taifa hili.
Mungu
anapenda sana watu wanaoomba, na kwa kweli anawatafuta. Lakini Mungu
anapendezwa zaidi na waliopondeka roho zao. Watu hawa hata kama hawana uwezo,
au wanaonekana kuwa si kitu mbele za watu, Mungu atawaheshimu, atawaangalia,
atavutwa kuja kwao, na kuhakikisha anakaa nao.
Mtu wa
aina hii, ni vyepesi kufundishwa na Mungu, ni vyepesi kufundishwa kupitia
watumishi wa Mungu, na kukubali kugeuka. Ni vyepesi kuwa tayari kufuata mapenzi
ya Mungu bila kujali nani anasema nini ikiwa ni Mungu amemwambia kwa ajili ya
utukufu wa Mungu.
Kama
kweli unahitaji kuwa na nafasi katika hili taifa miaka michache ijayo, na
unajiandaa au una ndoto ndani yako, Mungu ameweka ya kuwa mtu fulani, hakikisha
unashughulikia moyo wako.
4.
Mtu
anayejali mapenzi ya Mungu na maslahi ya wengine.
Hii
nayo ni sehemu nyingine inayomjenga mtu ambaye siku moja katika siku chache
zijazo, atatazamwa na wengi katika taifa hili kama jibu kwa kilio cha wengi, na
kama jibu la maswali mengi ya watu maishani kwa muda mrefu.
Ndugu
msomaji, Mungu anafanya kazi na watu wanaojali mapenzi yake. Mojawapo ya vitu
ambavyo vilimfanya Yesu afanye kazi kubwa sana na Mungu ya ukombozi, ni kuwa
alikuwa anapenda na kujali kufanya mapenzi ya Mungu. Ilifika mahali alisema chakula
chake ni mapenzi ya Mungu.
Inalazimu
ufike mahali ambako unayaelewa mapenzi ya Mungu, kisha yanakuwa chakula chako.
Yanakuwa kipaumbele chako cha maisha kiasi kwamba hakuna kitu cha kukutoa hapo.
Mtu wa Mungu, kama haujajifunza kutembea katika mapenzi ya Mungu, usitegemee
kuwa chochote katika hili taifa.
Haitoshi
kuwa na ndoto, ni lazima uelewe mapenzi ya Mungu katika nafasi anayokupa ili
utimize hicho. Lengo la Mungu kukuweka hapo ni kutimiza kitu fulani ambacho
ndiyo mapenzi yake. Kukamilisha ajenda fulani iliyopo kwenye moyo wake.
Mapenzi
ya Mungu yanahusisha mambo yote ambayo Mungu mwenyewe anayataka yafanyike
katika wakati fulani. Sasa ukitaka kutembea na Mungu, lazima uyajue mapenzi
yake. Lazima ujue anataka nini? Kwanini anataka anachokitaka? Kwanini anataka
ufanye kwa njia fulani na siyo nyingine? Mambo hayo ni machache kati ya mengi
ambayo unapaswa kuyafahamu mapema sana kipindi hiki bado hujawa kwenye nafasi,
siku ukisimama pale, mambo hayawi mageni kwako.
Kuna
watu wanajaribu kuanza kutafuta mapenzi ya Mungu kwa sababu wamekaa kwenye
nafasi fulani. Mtu wa Mungu kama siyo maisha yako kukaa kwenye mapenzi ya
Mungu, itakushinda maana itakuwa mzigo mzito usiouweza. Unapaswa kuanza leo,
hivi bado kabisa, ili hapo hapo, Mungu akusaidie kutembea katika mapenzi yake,
katika muda huu wa sasa, ili ikuandae kuweza kutembea na mapenzi yake katika
muda ule ujao.
Kuna
watu wapo kwenye nafasi mbalimbali za taifa hili, na wanafanya mambo ya ajabu
ajabu tu. Wanafanya hivi kwa sababu hawajui mapenzi ya Mungu kwenye nafasi
alizowapa ni zipi na kwanini? Hawajui chochote, wanachojua wao ni kuja na
mipango tu fulani fulani, ambayo mwisho wa siku, wanaishia kupoteza wengi.
Hakikisha kuwa unajifunza kuishi na kutembea katika mapenzi ya Mungu.
Vilevile,
unapaswa kujali maslahi ya wengi. Mungu hafanyi kazi na watu wabinafasi,
hafanyi kazi na watu wanaojijali wao wenyewe na familia zao. Mungu anafanya
kazi na watu wanaojali mambo ya wengine, watu wanaojali maisha ya wengine kuwa
salama katika hali njema. Huu ndiyo moyo wa Mungu, Mungu anajali maisha ya
wengine sana kiasi kwamba aliamua kumtoa mwanae wa pekee kwa ajili ya watu.
Siyo jambo rahisi.
Kutokuwa
mbinafsi, ni kuwa na moyo alionao Mungu juu ya watu. Ni kuwa na upendo alionao
Mungu juu ya watu. Kama hauhisi anavyohisi Mungu, haufikiri anavyofikiri Mungu
juu ya watu, hauwezi kufanya naye kazi hata kidogo. Amua kwa moyo wa dhati,
kubadilika, usijipendeze wewe. Yatoe maisha yako yawe sadaka kwa ajili ya
wengi, katika njia iliyo haki, isiyokiuka Neno la Mungu.
Ndugu
msomaji, ninatumaini kuwa umejifunza mambo mengi katika somo hili. Ukiyatazama
yote haya yanamhitaji Mungu. Unapaswa kukubali kusaidiwa na Mungu. Amua kumpa
Mungu nafasi ya kukutengeneza. Nakushauri kurudi kwenye chumba cha matengenezo
ili akusaidie uwe vile anavyohitaji uwe na aweze kufanya kazi na wewe.
Ndugu
msomaji, haya ni machache kati ya mengi. Nashauri uhakikisha upate nakala yako
ya kitabu kiitwacho MTU WA AINA HII NDIYE ATAKAYETAZAMWA KATIKA TANZANIA MPYA
na kama unahitaji, unaweza kutuma ujumbe wako kwa njia ya email kama
unavyooneshwa katika sehemu ya mawasiliano. Mungu akubariki sana, karibu tena
katika wikiendi ijayo.
Comments
Post a Comment
Thanks for your comment, God bless you!!!